HABARI

 

Wednesday, September 12, 2012

MAHAKAMA YA RUFAA KUSIKILIZA KESI YA MAWAZIRI WAWILI OKTOBA

0 Comments
ARUSHA, TANZANIA
Mahakama ya Rufaa ya Mahakama ya Kimataifa ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda (ICTR) itasikiliza kesi ya rufaa  inayowakabili mawaziri wawili wa zamani wa Rwanda, Justin Mugenzi na Prosper Mugiraneza Oktoba 8, 2012.

Kwa mujibu wa ratibu iliyotolewa Jumatatu, mawakili wa utetezi watakuwa wa kwanza kuwasilisha hoja zao na kufuatiwa na upande wa mashitaka ambao haukuwasilisha mbele ya mahakama hiyo rufaa yoyote katika kesi hiyo.

Mugenzi, aliyekuwa Waziri wa Biashara na Mugiraneza,Waziri wa zamani wa Utumishi wa Umma,wanapinga hukumu iliyotolewa na mahakama ya awali Septemba 30, 2011, ambapo walihukumiwa vifungo vya miaka 30 jela kila mmoja wao baada ya kutiwa hatiani kwa kula njama za kufanya mauaji kimbari na uchochezi wa mauaji hayo.

Majaji wa mahakama ya awali wamewakuta mawaziri hao wawili kuhusika na tukio la kumwondoa madarakani aliyekuwa mkuu wa mkoa wa Butare, Kusini mwa Rwanda Aprili 17, 1994 na nafasi yake kupewa mwingine siku mbili baadaye.

Walihitimisha kwamba kuondolewa kwa Mkuu wa Mkoa Jean-Baptiste Habyarimana kulikusudia kupunguza nguvu za kuzuia kufanyika kwa mauaji ya kimbari dhidi ya Watusti katika mkoa huo wa Butare.

Mawaziri hao awali walishitakiwa katika kesi moja na mawaziri wenzao wawili, Casimir Bizimungu (Afya) na Jerome Bicamumpaka (Mambo ya Nje) ambao waliachiwa huru kutokana na kukosekana kwa ushahidi wa kutosha.

0 Comments:

Post a Comment