HABARI

 

Monday, June 25, 2012

HOTUBA YA WAZIRI MKUU MIZENGO PINDA BUNGENI LEO

2 Comments
HOTUBA  YA  WAZIRI  MKUU,  MHESHIMIWA  MIZENGO  PETER  PINDA (MB),  KUHUSU MAPITIO NA MWELEKEO WA KAZI ZA SERIKALI NA MAKADIRIO YA MATUMIZI YA FEDHA YA OFISI YA WAZIRI MKUU NA OFISI YA BUNGE KWA MWAKA 2012/2013

UTANGULIZI


1.            Mheshimiwa Spika, naomba kutoa Hoja kwamba kutokana na Taarifa zilizowasilishwa leo ndani ya Bunge lako Tukufu na Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala na Kamati ya Fedha na Uchumi zilizochambua Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Bunge lako sasa lipokee na kujadili Taarifa ya Mapitio ya Utekelezaji wa Kazi za Serikali kwa mwaka 2011/2012 na Mwelekeo wa Kazi za Serikali kwa mwaka 2012/2013. Vilevile, naliomba Bunge lako Tukufu likubali kupitisha Makadirio ya Matumizi ya Fedha ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Taasisi zilizo chini yake pamoja na Ofisi ya Bunge kwa mwaka 2012/2013.

2.            Mheshimiwa Spika, tangu tulipohaitimisha Mkutano wa Bajeti  wa  Bunge hili mwaka jana, Nchi yetu imekumbwa na  Majanga  na Matukio mbalimbali yaliyosababisha vifo na  uharibifu  wa  mali.  Nitumie  fursa  hii  kutoa  pole    kwa  wote  waliofiwa  na  Ndugu, Jamaa na Marafiki. Mungu  azilaze  Roho za  Marehemu mahali Pema Peponi. Kwa ndugu zetu walioumia na bado wanajiuguza, tumwombe Mwenyezi Mungu awasaidie kupona haraka na kurejea katika shughuli za ujenzi wa Taifa.

3.            Mheshimiwa Spika, nijiunge na wenzangu waliotangulia kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge wapya, Mawaziri na Naibu Mawaziri walioteuliwa na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwezi Mei 2012. Aidha, napenda kumpongeza Mheshimiwa Mussa Zungu Azzan, Mbunge wa Ilala, kwa kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Bunge.  Nawapongeza  pia  Wenyeviti  na  Makamu  Wenyeviti  wa  Kamati  za  Kudumu  za Bunge  waliochaguliwa  kuchukua  nafasi zilizoachwa wazi. Vilevile, nawapongeza Waheshimiwa Wabunge waliochaguliwa na Bunge lako Tukufu kuiwakilisha Tanzania katika Bunge la Afrika Mashariki. Natarajia kwamba wote walioteuliwa na kuchaguliwa watatumia nafasi hizo kwa manufaa ya Bunge na kwa maendeleo ya Watanzania kwa ujumla.

4.            Mheshimiwa Spika, kwa takriban siku Tano Waheshimiwa Wabunge wamepata fursa  ya  kujadili  Taarifa  Kuhusu  Hali ya Uchumi  wa Taifa katika mwaka 2011,  Mpango wa Maendeleo wa Taifa na Bajeti ya Serikali  kwa  mwaka  2012/2013. Napenda kutoa Pongezi za dhati kwa Mheshimiwa Stephen Masatu Wasira (Mb.), Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mahusiano na Uratibu; na Mheshimiwa Dkt. William Augustao Mgimwa (Mb.), Waziri wa Fedha kwa Hotuba nzuri na ufafanuzi wa Hoja mbalimbali zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge. Vilevile, napenda kutoa shukrani zangu kwa Waheshimiwa Wabunge kwa kujadili kwa kina Hotuba hizo na hatimaye kupitisha Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2012/2013.

5.            Mheshimiwa Spika, kipekee, nitumie nafasi hii, kuwashukuru Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala inayoongozwa na Mheshimiwa Pindi Hazara Chana, Mbunge wa Viti Maalum. Nawashukuru pia Wajumbe wa Kamati ya Fedha na Uchumi inayoongozwa na Mheshimiwa Andrew John Chenge, Mbunge wa Bariadi Magharibi. Kamati hizo zimetoa mchango mkubwa wakati wa uchambuzi wa Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha ya Mafungu ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Mfuko wa Bunge. Aidha, nawashukuru Wajumbe wa Kamati zote za Kudumu za Bunge lako Tukufu kwa ushauri waliotoa wakati wa kupitia Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara, Mikoa, Wakala, Idara za Serikali Zinazojitegemea na Mamlaka za Serikali za Mitaa. Maoni na Ushauri wao utazingatiwa wakati wa utekelezaji wa Bajeti hii.

6.            Mheshimiwa Spika, Bajeti ya Serikali iliyopitishwa na Bunge ni mwendelezo wa utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2010. Vilevile, imezingatia Mpango wa Kwanza wa Maendeleo wa Miaka Mitano wa kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025, Malengo ya Maendeleo ya Milenia na Awamu ya Pili ya Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini. Katika mwaka 2012/2013, Serikali itaimarisha usimamizi wa utekelezaji wa Mipango na Miradi ya Maendeleo, matumizi ya fedha za Umma na uwajibikaji. Tutatumia rasilimali chache tulizonazo kwa kazi ambazo zitajielekeza kwenye shughuli za uzalishaji mali na kuongeza tija ili kuchochea ukuaji wa haraka wa uchumi.

 

HALI YA UCHUMI


7.            Mheshimiwa Spika, Pato la Taifa kwa mwaka 2011 lilikua kwa Asilimia 6.4 ikilinganishwa na Asilimia 7 mwaka 2010.  Ukuaji huo wa Asilimia 6.4 ni mkubwa ikilinganishwa na kiwango cha ukuaji wa uchumi wa Nchi za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara ambacho kilikuwa wastani wa Asilimia 5.1. Kushuka kwa kiwango cha ukuaji uchumi wetu kulichangiwa kwa kiasi kikubwa na ukame ambao uliathiri zaidi Sekta ya Kilimo na uzalishaji wa Nishati ya Umeme Nchini.  Tatizo la umeme, upungufu wa chakula katika baadhi ya maeneo Nchini pamoja na kupanda kwa bei ya mafuta katika Soko la Dunia vilichangia pia kuongezeka kwa mfumuko wa bei. Hatua zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali kudhibiti Mfumuko wa Bei ni pamoja na kurejesha upatikanaji wa umeme kwenye hali ya kawaida na kuimarisha ugavi wa chakula Nchini. Hatua hizo, zimeanza kupunguza kiwango cha Mfumuko wa Bei.  Ni vyema tukumbuke kwamba, hatua za kukabili tatizo la kiuchumi kama vile Mfumuko wa Bei zinapochukuliwa leo, matokeo yake hayawezi kuonekana siku hiyo hiyo. Wataalam wanaeleza kwamba mara nyingi inachukua miezi 6 hadi 18 kuona dhahiri matokeo ya hatua zilizochukuliwa. Hivyo, siku za usoni tutashuhudia Mfumuko wa Bei ukipungua zaidi.

Maboresho ya Sekta ya Fedha


8.              Mheshimiwa Spika, Taasisi za Fedha zina mchango mkubwa katika kuchochea kasi ya maendeleo na ukuaji wa Uchumi. Kwa kutambua mchango huo, Serikali inatekeleza Programu ya Maboresho ya Sekta ya Fedha, ambayo imekuwa na mafanikio ya kuridhisha.  Mafanikio hayo ni pamoja na kuongezeka kwa idadi ya Taasisi za Fedha ambazo hadi sasa zimefikia 49 zikiwa na Matawi 519 Nchini kote. Aidha, baadhi ya Taasisi hizo zimeonesha mafanikio makubwa katika eneo la huduma za Kibenki kwa njia ya mtandao.

9.              Mheshimiwa Spika, Serikali pia imetoa msukumo wa uanzishaji wa huduma za Kifedha kupitia Vyama vya Kuweka na Kukopa (SACCOs) ambavyo hadi sasa vimefikia 5,346. Vyama hivyo vimetoa mikopo yenye thamani ya Shilingi Bilioni 627.2. Pamoja na mafanikio hayo, changamoto kubwa inayoikabili Sekta ya Fedha ni viwango  vikubwa vya  riba kwenye Mikopo vinavyoendelea kutozwa  na Benki za Biashara ikilinganishwa na riba ndogo inayolipwa kwa amana. Changamoto nyingine ni kukosekana  kwa  Taasisi nyingi za fedha zinazotoa Mikopo ya  muda  mrefu  yenye  masharti  nafuu kwa Miradi   ya   Maendeleo   hasa   kwenye  Sekta   ya  Kilimo. Serikali inatambua Changamoto hizo na tayari Mikakati inaandaliwa kukabiliana nazo hususan kuanzisha Dirisha la Kilimo katika Benki ya Rasilimali Tanzania pamoja na kukamilisha mchakato wa kuanzisha Benki ya Maendeleo ya Kilimo. Aidha, Serikali inaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji pamoja na kuanzisha Mfumo wa kuwatambua wakopaji (Credit Reference Bureau).

 

SENSA YA WATU NA MAKAZI 2012


10.         Mheshimiwa Spika, katika hotuba zangu za Bajeti za miaka Miwili iliyopita, nililijulisha Bunge lako Tukufu kuhusu maandalizi ya Sensa ya Watu na Makazi ambayo itafanyika tarehe 26 Agosti 2012. Nilianza kutoa Taarifa ya Sensa mapema kwa kuwa Sensa ni mchakato unaohitaji maandalizi ya muda mrefu kabla na baada ya zoezi lenyewe la kuhesabu Watu. Kwa kutambua umuhimu wa Sensa katika kuandaa na kutekeleza Mipango ya Maendeleo ya Nchi, zoezi hili limepewa kipaumbele cha pekee katika Bajeti ya Serikali ya mwaka 2012/2013. Katika Awamu ya Kwanza ya maandalizi ya Sensa, kazi zilizofanyika ni pamoja na kutenga maeneo ya kuhesabia Watu, kutayarisha Madodoso na Miongozo mbalimbali, kufanya Sensa ya Majaribio, kununua vitendea kazi, kuchapisha Nyaraka za Sensa na kuunda Kamati za Sensa za Mikoa na Wilaya.

11.         Mheshimiwa Spika, kazi za Sensa zinazoendelea ni uhamasishaji na kutoa Elimu kwa Umma ili kila Mwananchi ashiriki kikamilifu katika zoezi hilo. Shughuli nyingine ni utoaji wa mafunzo kwa watakaokuwa Makarani wa Kuhesabu Watu na Wasimamizi, usambazaji wa Vifaa na Maandalizi ya kuingiza takwimu kwenye Kompyuta. Katika utekelezaji wa zoezi hili, Serikali itawatumia Watumishi mbalimbali wa Serikali wakiwemo Walimu. Kutokana na sababu hiyo, Serikali imelazimika kubadili mihula ya Shule ili Walimu waweze kusaidia katika zoezi hili la Sensa.

12.          Mheshimiwa Spika, nawaomba Viongozi wote tusaidiane kuhamasisha na kusimamia utekelezaji wa zoezi la Sensa katika maeneo yetu. Nawaomba Wananchi wote washiriki katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi kwa kutoa ushirikiano na taarifa sahihi kwa Makarani wa Sensa na Wasimamizi ambao watatembelea Kaya zetu tarehe 26 Agosti 2012. Niwahakikishie Wananchi wote, kuwa taarifa zote zinazokusanywa wakati wa Sensa ni Siri na zitatumika kwa shughuli za Kitakwimu tu. Takwimu hizo hazina uhusiano na Dini, Kodi, Siasa au mambo mengine kama hayo ambayo hayakukusudiwa.

KUIMARISHA DEMOKRASIA NA MUUNGANO

Hali ya Siasa


13.         Mheshimiwa Spika, kumekuwa na mwamko mkubwa wa Wananchi kushiriki kwenye masuala ya Kisiasa hali inayoashiria kukua kwa Demokrasia Nchini. Vyama vipya vya Siasa vimeendelea kusajiliwa na vilivyopo kujiimarisha zaidi. Katika mwaka 2011/2012, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa imepokea maombi ya kusajili Vyama vipya Viwili vya Siasa. Chama cha Kijamii (CCK) kimepata Usajili wa Kudumu na kufanya idadi ya Vyama vyenye Usajili wa Kudumu kufikia 19. Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC) kimepata Usajili wa muda na Chama cha Movement for Democratic and Economic Change kinaendelea kufanyiwa uhakiki.

14.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2012/2013, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa itaendelea kushughulikia maombi ya Usajili wa Vyama, kuendelea kutoa elimu kwa Wananchi kuhusu mfumo wa Vyama vingi vya Siasa na Sheria ya Gharama za Uchaguzi ya mwaka 2010. Aidha, itafuatilia uhai wa Vyama vya Siasa kwa mujibu wa Sheria na kuanzisha Ofisi mbili za Kanda. Kanda hizo ni ile ya Kusini inayojumuisha Mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma na Kanda ya Magharibi inayojumuisha Mikoa ya Tabora, Kigoma, Shinyanga na Katavi. Nitumie nafasi hii kuwasihi Watanzania kutumia fursa ya kupanuka kwa Demokrasia kuendelea kushiriki kwenye Siasa kwa kufuata Sheria, Kanuni na Taratibu za Nchi. Viongozi wa Vyama vya Siasa waonyeshe mfano wa kuendesha Siasa za kistaarabu zenye lengo la kuunganisha Watanzania na siyo kuwachonganisha. Hakuna Nchi au Kiongozi aliyewahi kupata sifa nzuri kwa kuwa chanzo cha mifarakano. Tudumishe utulivu na amani pamoja na ustaarabu wetu wa Kitanzania.

Mabadiliko ya Katiba


15.         Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge watakumbuka kuwa katika Mkutano wa Tano wa Bunge, mwezi Novemba 2011, Bunge lako Tukufu lilipitisha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba Na. 8 ya Mwaka 2011 (Sura ya 83). Aidha, Bunge lilifanya marekebisho ya Sheria hiyo katika Mkutano wa Sita, mwezi Februari 2012. Hatua hiyo, ilimwezesha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania baada ya kushauriana na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, kuteua Wajumbe wa Tume itakayoratibu na kukusanya Maoni ya Wananchi kuhusu Mabadiliko ya Katiba. Tume hiyo yenye Wajumbe 32 inajumuisha Wawakilishi wa Makundi mbalimbali katika jamii kutoka pande mbili za Muungano.

16.         Mheshimiwa Spika, Tume imeanza kazi rasmi tarehe 1 Mei 2012, kama ilivyopangwa. Serikali imefanya maandalizi muhimu kuiwezesha Tume kufanya kazi yake ipasavyo ikiwa ni pamoja na kuipatia Vifaa vya Kisasa vya kukusanya na Kutunza Kumbukumbu na kufungua Tovuti rasmi. Aidha, Idara ya Mpigachapa Mkuu wa Serikali imepewa jukumu la kuchapisha kwa wingi Katiba na Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ili Wananchi waweze kuelewa na kutoa michango yao kwa uhakika zaidi kwenye mchakato wa kutoa maoni.

17.         Mheshimiwa Spika, napenda nichukue fursa hii tena kumpongeza  Mheshimiwa Jaji Joseph Sinde Warioba, Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais Mstaafu kwa kuteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba na Mheshimiwa Augustino Ramadhani, Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania kwa kuteuliwa kuwa Makamu Mwenyekiti. Vilevile, napenda kuwapongeza Wajumbe wote, wakiwemo Katibu na Naibu Katibu kwa kuteuliwa kuunda Tume hiyo. Napenda kuwasihi Wananchi wajitokeze kwa wingi na kutoa maoni yao kwa utulivu katika Mikutano itakayoitishwa na Tume na kuwapa Wajumbe ushirikiano wa kutosha ili hatimaye tupate Katiba iliyoandikwa na Watanzania wenyewe. 

 

Muungano


18.          Mheshimiwa Spika, tarehe 26 Aprili 2012, Muungano wetu ulitimiza Miaka 48 ya Watanzania kuishi pamoja, kwa amani na utulivu. Katika mwaka 2011/2012, Vikao 14 vya Kisekta vya Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Serikali ya Muungano wa Tanzania (SMT) na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) vilifanyika  kutafuta ufumbuzi wa changamoto za Muungano. Kikao cha Kamati ya Pamoja cha SMT na SMZ, chini ya Uenyekiti wa Makamu wa Rais, Mheshimiwa  Dkt.  Mohamed  Gharib Bilal, kilifanyika ambapo Hoja 13 zilijadiliwa na Hoja Mbili zilipatiwa ufumbuzi. Hoja zilizopatiwa ufumbuzi ni kuhusu ongezeko kubwa la Ankara za umeme kutoka TANESCO kwenda ZECO na Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo. Aidha, imekubalika kuwa marekebisho ya Sheria yafanyike mapema ili kupata ufumbuzi katika hoja zinazohusu Usajili wa Vyombo vya Moto, Kodi ya Mapato na Kodi ya Zuio (Withholding Tax).

19.         Mheshimiwa Spika, Hoja nyingine ambazo zipo katika hatua mbalimbali za kutafutiwa ufumbuzi zitaendelea kujadiliwa  katika  Vikao  vya  Kamati ya pamoja vya Kisekta na  Kamati ya Pamoja. Serikali pia itaendelea kuratibu masuala yasiyo ya Muungano kwa kuhakikisha kwamba Sekta, Wizara na Asasi Zisizo za Muungano zinakutana na kujadili changamoto zilizopo. Ni ukweli usiopingika kwamba, Muungano wowote Duniani unakutana na changamoto mbalimbali. Jambo muhimu ni pande zote zinazounda Muungano kuzitatua changamoto hizo. Hivyo, ni vyema tukaendelea kukaa pamoja na kujadiliana ili Muungano wetu huu ambao msingi wake ni mahusiano ya kihistoria ya pande zote mbili uendelee kudumu kwa faida ya watu wetu.

 

BUNGE


20.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/2012, Bunge limetekeleza kwa ufanisi majukumu yake ya msingi ya kutunga Sheria na kuisimamia Serikali. Kamati za Kudumu za Bunge pia zimetekeleza majukumu yake ipasavyo na Bunge zima limefanya Mikutano Minne kwa mujibu wa Sheria. Katika Mikutano mitatu iliyofanyika, Miswada ya Sheria Nane (8) ilipitishwa na Maswali ya kawaida 373 na ya Nyongeza 894 ya Waheshimiwa Wabunge yalijibiwa na Serikali. Aidha, Maswali ya Msingi 78 ya Papo kwa Papo kwa Waziri Mkuu yaliulizwa na kujibiwa.  Hoja mbalimbali za Kamati za Kudumu za Bunge ziliwasilishwa na kujadiliwa. 

21.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2012/2013, Ofisi ya Bunge itakarabati Ukumbi wa Bunge na kuboresha miundombinu mingine ya Ofisi zake ikiwa ni pamoja na kuweka Vifaa vya Mawasiliano na kuendelea na ujenzi wa Ofisi za Wabunge katika Majimbo. Aidha, huduma za Utafiti na Sheria zitaimarishwa sambamba na shughuli za Kamati za Kudumu za Bunge.

MAENDELEO YA SEKTA BINAFSI, UWEKEZAJI NA UWEZESHAJI


Maendeleo ya Sekta Binafsi


22.         Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuweka mazingira wezeshi kwa Sekta Binafsi ili iweze kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji mali na kufanya biashara  na  hatimaye  kuwa  Injini  ya  Ukuaji  wa Uchumi. Katika kufanikisha lengo hilo, Serikali inasimamia utekelezaji wa Mpango Kazi wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji Nchini wenye lengo la kurekebisha mifumo iliyopo ili kupunguza gharama za kufanya biashara na kuwekeza Nchini. Hatua zilizochukuliwa ni pamoja na uanzishaji wa Kituo Kimoja cha Utoaji wa Huduma kwenye Bandari ya Dar es Salaam, ambapo muda wa mizigo kukaa Bandarini umepungua kutoka wastani wa Siku 25 mwaka 2009 hadi kufikia wastani wa Siku 9 mwezi Mei 2012.

23.         Mheshimiwa Spika, hatua nyingine ni kupunguza Vizuizi vya Kudumu katika Barabara Kuu, kuunda Kamati za pamoja kwenye Vituo vya Mipakani mwa Nchi (Joint Border Post Committees), kuendelea na taratibu za kuanzishwa kwa Vituo vya Utoaji Huduma kwa Pamoja Mipakani (One Stop Border Posts) na kuweka mkazo kwenye matumizi ya Mfumo wa Kielektroniki kwenye maeneo ya  ulipaji Kodi, Mabenki, Usajili wa Makampuni na utunzaji  wa kumbukumbu  kwenye  Masjala mbalimbali. Sambamba na hatua hizo, majadiliano na Sekta Binafsi yamefanyika kwa lengo la kupata ufumbuzi wa changamoto za Kisera, Kisheria na Mifumo ya Kitaasisi zinazoikabili Sekta hiyo.  Katika mwaka 2012/2013, Serikali itafanya tafiti zinazohusiana na maendeleo ya Sekta Binafsi, pamoja na kuendeleza mashauriano na Sekta Binafsi, Washirika wa Maendeleo na Taasisi Zisizo za Serikali kwa lengo la kuiwezesha Sekta Binafsi kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi

Uwekezaji


24.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/2012, Serikali imefanya juhudi kubwa za kuhamasisha na kuvutia Wawekezaji wa Ndani na Nje. Kutokana na juhudi hizo, Kituo cha Uwekezaji Nchini kilisajili jumla ya Miradi 681 yenye thamani ya Shilingi Trilioni 11.6 na fursa za Ajira 89,803. Kati ya Miradi iliyosajiliwa, Miradi 356 sawa na Asilimia 52.3 ni ya Wawekezaji wa Ndani, Miradi 166, sawa na Asilimia 24.4 ni ya Ubia kati ya Wawekezaji wa Ndani na Nje na Miradi 159, sawa na Asilimia 23.3 ni ya Wawekezaji wa Nje. Mitaji ya moja kwa moja ya Wawekezaji wa Nje (FDI), iliyoingizwa Nchini imeongezeka kutoka Shilingi Bilioni 681.2 mwaka 2010 hadi Trilioni 1.3 mwaka 2011.

25.         Mheshimiwa Spika, katika jitihada za kuongeza kasi ya Uwekezaji Nchini kupitia Sera ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi, Serikali imefanya maandalizi ya msingi ya kuanzisha Kitengo cha Uratibu wa masuala ya Ubia kwenye Kituo cha Uwekezaji na Kitengo cha Fedha (PPP – Finance Unit) kwenye Wizara ya Fedha. Jumla ya Miradi 125 iliyoainishwa na Wizara mbalimbali itafanyiwa uchambuzi zaidi na Vitengo hivi ili kubaini kama inakidhi vigezo vya kutekelezwa chini ya utaratibu wa Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi. Miradi hiyo ni pamoja na ile ya kuzalisha umeme, ujenzi wa barabara, reli, bandari, na ujenzi wa majengo kwa ajili ya Ofisi na biashara.

26.         Mheshimiwa Spika, Serikali imeweka umuhimu wa kipekee kuhamasisha ushiriki wa Wawekezaji wa Kitanzania  kuanzisha  Miradi ya Uwekezaji katika Mikoa na Wilaya kwa kuandaa Makongamano na Mikutano ya Kuhamasisha Uwekezaji  na kutoa elimu ya ujasiriamali kwa Wawekezaji Wadogo. Hadi sasa, Mikutano ya kuhamasisha Uwekezaji imefanyika katika Mikoa ya Ukanda wa Ziwa Tanganyika ya Rukwa, Katavi na Kigoma pamoja na Mikoa ya Mara, Singida, Arusha na Mbeya. Aidha, Wilaya za Mbinga, Njombe, Mufindi, Mbozi na Kahama nazo zimefanya Mikutano hiyo. Mikutano ya Kikanda ya Uwekezaji itaendelea kufanyika katika mwaka 2012/2013. Nahimiza, Viongozi wa Mikoa na Wilaya kuandaa Mikutano hiyo na kuondoa Vikwazo vinavyokwamisha uwekezaji katika maeneo yao. Ofisi ya Waziri Mkuu itasambaza Mwongozo kwa Mikoa ili ishirikiane ipasavyo na Mamlaka za Serikali za Mitaa kuandaa Mikutano ya Uwekezaji.

27.         Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kushiriki katika Mikutano mbalimbali inayohusu masuala ya uchumi, biashara na uwekezaji. Mwezi Mei 2012, Tanzania ilishiriki katika Mkutano  wa  World Economic Forum – Addis Ababa na baadaye katika Mkutano wa Nchi Nane Zilizoendelea katika Viwanda (G8) huko Washington, Marekani. Katika mikutano hiyo, Serikali ilielezea Mipango yetu ya kuleta Mapinduzi ya Kilimo Nchini, hususan Mpango  wa  Kukuza  Kilimo  katika Ukanda wa Kusini mwa Tanzania (Southern Agricultural Growth Corridor of Tanzania – SAGCOT). Mipango hiyo ilipokelewa na kukubalika ambapo Tanzania imeingizwa katika Mpango wa G8 wa Kuendeleza Kilimo Barani Afrika. Nchi nyingine Barani Afrika zilizokubalika kushiriki katika Mpango huo ujulikanao kama G8 The New Alliance for Food Security and Nutrition ni Ethiopia na Ghana. Chini Mpango huu, Tanzania itanufaika na misaada ya Shilingi Trilioni 1.41 kwa ajili ya kuwekeza katika Sekta ya Kilimo katika kipindi cha miaka mitano ijayo.

28.         Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii kumshukuru  Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Uongozi wake  Mahiri  na  juhudi  zake  za kuhakikisha  kwamba Nchi yetu inakuwa moja ya Nchi Tatu Barani Afrika zitakazonufaika na Mpango huo. Hii inathibitisha kuwa ziara za Mheshimiwa Rais Nje ya Nchi mara nyingi zina manufaa makubwa kwa uchumi na maendeleo ya Nchi yetu.

29.         Mheshimiwa Spika, maandalizi ya kuainisha Miradi itakayotekelezwa na Wawekezaji wa Ndani na Nje katika Ukanda wa SAGCOT yameanza. Kutokana na ukubwa wa ukanda huo wa Kilimo, Miradi itakayoainishwa itatekelezwa kwa Mfumo wa Kongano (Clusters) ambapo Wakulima Wadogo watashirikiana na Wawekezaji Wakubwa kuendeleza Kilimo.

30.         Mheshimiwa Spika, tumeanza kuona matunda mazuri yaliyotokana na ushirikiano kati ya Wawekezaji Wakubwa na Wakulima Wadogo katika kuongeza uzalishaji na tija. Hali hii imejionesha  dhahiri kwenye Kilimo cha Mpunga huko Kilombero ambapo Kampuni ya Kilombero Plantations Limited iliyowekeza  kwenye Shamba la Mngeta Wilayani Kilombero imewasaidia Wakulima Wadogo kupata Teknolojia rahisi ya kupanda na kupalilia mpunga. Wakulima  hao wamewezeshwa kuanzisha vikundi vya uzalishaji na kukopeshwa mbegu bora. Kutokana na ushirikiano huo, uzalishaji wa mpunga kwa Wakulima Wadogo umeongezeka kutoka wastani wa Tani Mbili hadi Tani Saba kwa Hekta moja. Utaratibu wa namna hiyo pia unatumiwa na Mwekezaji wa Kampuni ya Sukari Kilombero na umewanufaisha Wakulima Wadogo wa Miwa Wilayani  Kilombero  kupitia  vikundi   vyao   vya  uzalishaji. Ushirikiano wa aina hiyo unatoa fursa za Masoko na Usindikaji wa Mazao yanayozalishwa na Wakulima Wadogo wanaozunguka mashamba ya Wawekezaji Wakubwa. Hii ni dalili njema kabisa na mfano wa kuigwa na Wawekezaji Wakubwa na Wakulima Wadogo Nchini.

31.         Mheshimiwa Spika, natoa wito kwa Watanzania wenzangu kuona  uwekezaji mkubwa katika Kilimo kama fursa muhimu ya kuongeza uzalishaji na tija. Jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba maslahi ya Wakulima Wadogo yanalindwa kwa kuwekeana mikataba mizuri na kufuatilia utekelezaji wake. Ni imani yangu kwamba, tukiitumia vizuri ardhi yenye rutuba tuliyonayo tutaweza kuongeza ukuaji kwenye Sekta ya Kilimo ambayo ni tegemeo kwa Watanzania wengi na hatimaye kupunguza Umaskini wa Kipato.

Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi


32.         Mheshimiwa Spika, Serikali  kupitia  Baraza la Taifa la  Uwezeshaji  Wananchi  Kiuchumi imeendelea kusimamia na kuratibu utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ya mwaka 2004 kupitia Programu  na  Mifuko  mbalimbali.  Hadi kufikia mwezi Aprili 2012, Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (Mwananchi Empowerment Fund), umetoa mikopo yenye thamani ya Shilingi Bilioni 7.3 kwa Wajasiriamali 7,187 katika Mikoa ya Dodoma, Lindi, Manyara, Mtwara, Pwani, Rukwa, Ruvuma, Singida na Tanga. Sehemu kubwa ya Mikopo iliyotolewa ilitumika kugharamia shughuli za Kilimo ikijumuisha ununuzi wa Pembejeo na Zana za Kisasa za Kilimo na Umwagiliaji.

33.         Mheshimiwa Spika, kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF), katika mwaka 2011/2012, Miradi 878 yenye thamani ya Shilingi Bilioni 18.6 iliyoibuliwa na Wananchi kwenye Halmashauri zote Tanzania Bara na Zanzibar ilitekelezwa. Vilevile, hadi kufikia Desemba 2011, Mfuko huo umetoa Shilingi Bilioni 1.14 kwa Walengwa 14,000 kupitia Utaratibu wa Uhawilishaji Fedha katika Kaya Maskini. Aidha, Mafunzo ya Ujasiriamali yametolewa kwa Vikundi 500 Nchini katika Wilaya za Tanzania Bara na Zanzibar. Vilevile, Wajumbe 8,780 wa Kamati za Usimamizi wa Mradi na 13,500 wa Kamati za Serikali za Vijiji na Mitaa walipata mafunzo.

34.         Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha 2012/2013, Serikali  itaanza  utekelezaji wa Awamu ya Tatu ya TASAF. Benki  ya  Dunia  imepitisha  Shilingi  Bilioni  345.4 kwa ajili ya utekelezaji wa Mpango huo utakaotekelezwa kwa kipindi cha Miaka Mitatu. Serikali pia itasimamia Mifuko ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ili Wajasiriamali wengi zaidi wanufaike. Aidha, Serikali itawahamasisha Wananchi kuweka akiba, kuwekeza na kutambua na kutumia fursa za kiuchumi zilizopo ili kuongeza kipato na ajira.

SEKTA ZA UZALISHAJI


Kilimo


35.         Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kuwa mkakati wa kuhimiza Kilimo cha Kisasa kinachotumia Kanuni Bora za Kilimo, Zana za Kisasa na msukumo kwenye Kilimo cha Umwagiliaji ndiyo njia ya uhakika ya kuongeza uzalishaji na tija katika kilimo. Aidha, ushirikiano baina ya Serikali na Sekta Binafsi ni nguzo muhimu ya kuleta Mapinduzi ya Kilimo. Jitihada za Serikali katika mwaka 2011/2012 zilielekezwa katika vipaumbele hivyo pamoja na kuongeza upatikanaji na matumizi ya Pembejeo na Zana Bora za Kilimo.

Pembejeo na Zana za Kilimo


36.         Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2011/2012, Serikali iliimarisha upatikanaji wa Pembejeo za Kilimo hasa Mbolea, Mbegu Bora na Madawa ya Mimea. Jumla ya Vocha Milioni 5.3 za Ruzuku ya Pembejeo za Kilimo zilisambazwa kwa Kaya  Milioni 2 Nchini. Lengo la Serikali ni kuongeza upatikanaji wa Pembejeo ili kuwanufaisha Wakulima wengi waweze kuongeza tija, uzalishaji na kipato. Kama nilivyoahidi kwenye Hotuba yangu ya mwaka 2011/2012, tayari Serikali imefanya ukaguzi maalum kuhusu utoaji wa Ruzuku za Pembejeo kwenye Kilimo kwa utaratibu wa Vocha. Kutokana na matokeo ya awali ya ukaguzi huo, TAKUKURU imefungua Kesi 19 kwa wale waliobainika kufanya Ubadhirifu na Udanganyifu katika utoaji wa Vocha za Pembejeo za Kilimo. Pamoja na hatua hiyo, Serikali itaboresha  mfumo wa sasa wa utoaji wa Vocha za Pembejeo kwa kubuni Mfumo mwingine ambao utaondoa upungufu uliojitokeza katika mfumo unaotumika hivi sasa. Lengo ni kuhakikisha kwamba Vocha zinawafikia walengwa kwa wakati na zinatumika kwa madhumuni yaliyopangwa.

37.         Mheshimiwa Spika, itakumbukwa kwamba, Serikali kupitia SUMA JKT iliingiza Nchini Matrekta Makubwa 1,860 na Zana zake; Matrekta Madogo ya Mkono  400 na Pampu za Umwagiliaji 1,100 kupitia Mkopo wenye Masharti Nafuu kutoka Serikali ya India. Ili kuwawezesha Wakulima wengi zaidi kumudu bei ya Matrekta hayo, Serikali imeamua kupunguza bei ya Matrekta hayo kwa kiasi kikubwa. Kwa mfano, bei ya Trekta Moja la Horse Power 50 imepunguzwa kutoka Shilingi Milioni 25.6 hadi Milioni 16.5 na  Trekta  la Horse Power 70 imepunguzwa kutoka Shilingi Milioni 45.8 hadi Milioni 38.8. Natoa wito kwa Halmashauri, Vyama vya Ushirika, Vikundi vya Wakulima na Wananchi kutumia fursa hii kununua Matrekta hayo. Aidha, jana baada ya kushauriana na Halmashauri husika tuliafikiana kuwa Halmashauri ziangalie uwezekano wa kuwapunguzia zaidi Wakulima kiwango cha Asilimia 30 wanachotakiwa kuchangia katika ununuzi wa Matrekta ya SUMA JKT ili waweze kupata Matrekta hayo kwa bei nafuu zaidi. Lengo ni kuhakikisha kuwa Matrekta hayo yanawafikia Wakulima wengi.

 

Umwagiliaji


38.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/2012, Serikali imekarabati Miundombinu ya Skimu 32 za umwagiliaji zenye  ukubwa  wa  Hekta  17,824.  Aidha, kazi  ya  ujenzi wa  Mabwawa 8  ya Maji  inaendelea  na Upembuzi Yakinifu wa Miradi 25  ya Umwagiliaji yenye  eneo la Hekta 17,113  umefanyika. Kutokana na juhudi hizo, eneo la umwagiliaji Nchini limeongezeka kutoka Hekta 331,490 mwaka 2010/2011, hadi Hekta 345,690 mwaka 2011/2012. Katika mwaka 2012/2013, Serikali itashirikiana na Wadau wa Maendeleo kuwawezesha Wakulima 33,108 katika Skimu 20 za Umwagiliaji zenye Hekta 15,431 kulima zao la Mpunga kibiashara kwa kutumia Teknolojia za Kisasa.

 

Mifugo


39.         Mheshimiwa Spika, Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2010 ilielekeza Serikali iandae Programu Kabambe ya Kuendeleza Sekta ya Mifugo ambayo itajumuisha uendelezaji wa Malisho, kuchimba na kujenga Malambo, Mabwawa na Majosho na huduma za Ugani ili hatimaye Wafugaji waondokane na ufugaji wa kuhamahama. Katika kutekeleza maelekezo hayo, Serikali kwa kushirikiana na Wadau wa Sekta ya Mifugo imeandaa Programu ya Kuendeleza Sekta ya Mifugo. Kukamilika kwa Programu hii kutaiwezesha Sekta ya Mifugo kutoa mchango zaidi kwenye Pato la Taifa na kuwanufaisha Wafugaji. Mafanikio ya Programu hii yatategemea sana Wadau wa Sekta ya Mifugo kuzingatia Sheria Na. 13 ya Mwaka 2011 iliyopitishwa na Bunge lako inayohusu Maeneo ya Malisho na Rasilimali ya Vyakula vya Mifugo. Nawahakikishia Wananchi kwamba Serikali itasimamia kikamilifu utekelezaji wa Sheria hii pamoja na Programu ya Kuendeleza Sekta ya Mifugo, ili kuleta mabadiliko kutoka kwenye Uchungaji kwenda kwenye Ufugaji wa Kisasa.

40.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/2012, Serikali imetoa Ruzuku ya Shilingi Bilioni 1.6 zilizotumika kununua na kusambaza lita 62,500 za Dawa za Kuogesha Mifugo na Dozi Milioni 3.5 za Chanjo ya Ugonjwa wa Homa ya Mapafu ya Ng’ombe katika Halmashauri zote Nchini. Serikali pia imeendelea kushirikiana na Wadau mbalimbali kujenga na kukarabati Majosho 108 na  Malambo 98. Aidha, Kituo cha Taifa cha Uhamilishaji kilichopo Usa River, Arusha pamoja na Vituo Vitano vya Kanda vya Afya ya Mifugo vimeimarishwa. Serikali itaendelea kutoa Ruzuku ya Dawa za Mifugo na kuhamasisha Wafugaji na Wafanyabiashara kuwekeza zaidi kwenye Ufugaji wa Kisasa na unenepeshaji Mifugo.

 

Uvuvi


41.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/2012, Serikali ilianza kutekeleza Mkakati wa Uendelezaji Ukuzaji Viumbe kwenye Maji kwa kuimarisha Ufugaji Samaki na ukuzaji wa Viumbe vingine. Utekelezaji wa Mkakati huo, umeongeza idadi ya Mabwawa ya Kufugia Samaki kutoka 19,039 mwaka  2010/2011 hadi 19,443 mwaka 2011/2012, na Vituo  vya Kuzalisha Vifaranga vimeongezeka kutoka 8 hadi  10  ambapo jumla ya Vifaranga Milioni 1.9 vya Samaki  vimezalishwa  na kusambazwa kwa Wadau. Aidha, elimu ya usimamizi na matumizi endelevu ya Rasilimali za Uvuvi imetolewa katika maeneo ya Wavuvi. Vikundi 188 vilihamasishwa kufanya shughuli mbadala kwa kupatiwa elimu ya ujasiriamali ambapo Miradi Midogo 459 ya kiuchumi imeanzishwa. Katika mwaka 2012/2013, Serikali itafanya Mapitio ya Sera ya Taifa ya Uvuvi ya mwaka 1997 na kuandaa Mkakati wa utekelezaji.

Ufugaji Nyuki


42.         Mheshimiwa Spika, Sekta ya Ufugaji Nyuki ina mchango mkubwa katika kuondoa Umaskini na kuhifadhi mazingira. Kwa kuzingatia fursa kubwa tuliyonayo ya Rasilimali za Ufugaji Nyuki, Serikali imeziagiza Mamlaka za Serikali za Mitaa zote Nchini kuanzisha Mashamba Darasa ya kutoa Elimu ya Ufugaji Nyuki. Katika mwaka 2011/2012, jumla ya Wafugaji Nyuki 4,573 kutoka Wilaya 33 walipewa mafunzo ya Ufugaji Bora wa Nyuki. Aidha, Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wamepewa mafunzo kuhusu Ufugaji Bora wa Nyuki ili waweze kuwa chachu ya uhamasishaji katika Mikoa na Wilaya kuhusu manufaa ya Ufugaji Nyuki. Kutokana na jitihada hizo, katika mwaka  2011/2012, uzalishaji wa Asali ulifikia Tani 9,000 zenye thamani ya Shilingi Bilioni 27 na Nta iliyozalishwa ilikuwa Tani 600 zenye thamani ya Shilingi Bilioni 3. Aidha, tarehe 9 Juni, 2012 nilipata fursa ya kufungua Kiwanda kipya na cha Kisasa cha Kuchakata Asali kilichojengwa na Kampuni ya Honey King Limited katika Kijiji cha Visiga Mkoani Pwani na hivyo kufanya jumla ya Viwanda vya kuchakata na kufungasha Asali  Nchini kufikia Vinane. Napenda kuwapongeza Wawekezaji hao kwa kujenga Kiwanda chenye uwezo wa Kuchakata Tani 10,000 za Asali kwa mwaka. Nawaomba Wafugaji Nyuki kuitumia vizuri fursa hii kwa kuzalisha Mazao ya Nyuki kwa wingi na yenye ubora ili kunufaika na Soko la kuaminika la Kiwanda hicho na vingine vilivyopo hapa Nchini.

43.          Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2012/2013, Serikali itaendelea kutoa elimu ya Ufugaji Nyuki kwa Wadau  mbalimbali.  Aidha, ili kutangaza Ubora wa Asali na Nta  ya  Nchi  yetu, yatafanyika  Maonyesho  Maalum  ya Mazao ya Ufugaji Nyuki mwezi Oktoba 2012. Maonyesho hayo yataandaliwa kwa ushirikiano baina ya Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Viwanda na Biashara, Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania na Wadau wengine.

Miundombinu ya Masoko, Uongezaji Thamani Mazao na Huduma za Kifedha Vijijini


44.         Mheshimiwa Spika, Serikali ilianza utekelezaji wa Programu ya Miundombinu ya Masoko, Uongezaji Thamani Mazao na Huduma za Kifedha Vijijini (Marketing Infrastructure Value Addition and Rural Finance Program - MIVARF) mwezi Julai, 2011. Kazi zilizotekelezwa ni pamoja na kuandaa mfumo wa utekelezaji ikiwemo uundaji wa Kamati za Usimamizi, ununuzi wa Vitendea Kazi, kuajiri wafanyakazi na kuitambulisha Programu katika Mikoa yote. Aidha, uchambuzi wa Maandiko ya Miradi iliyopokelewa kutoka Halmashauri mbalimbali umefanyika na Halmashauri zitakazoanza kushiriki katika utekekezaji wa Programu zimechaguliwa.

45.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2012/2013, Kilometa 250 za barabara za vjijini zitakarabatiwa, maghala mawili yatajengwa na manne yatakarabatiwa. Vilevile, vituo vinne vya mafunzo ya uongezaji thamani mazao vitakarabatiwa; Wakulima watapatiwa mafunzo kuhusu hifadhi ya mazao, mbinu za kuyafikia masoko na Mfumo wa Stakabadhi ya Mazao Ghalani. Kazi nyingine zitakazofanyika ni kuviendeleza Vikundi 864 vya Kifedha vikiwemo VICOBA, kuzijengea uwezo SACCOS 108 pamoja na Asasi nyingine ndogo za Kifedha ili ziweze kutoa Huduma za Kifedha Vijijini kwa ufanisi zaidi.

Viwanda


46.         Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua mchango na umuhimu wa Sekta ya Viwanda katika kuleta maendeleo endelevu, kuongeza ajira, kuongeza thamani ya Mazao, Kukuza Masoko, kuongeza Mapato ya Serikali na fedha za kigeni. Kwa kuzingatia umuhimu huo, hatua zilizochukuliwa ni pamoja na uhamasishaji wa Uwekezaji wa Viwanda Vipya katika Maeneo Maalum ya Uzalishaji (EPZ) na Maeneo Maalum ya Uchumi (SEZ). Idadi ya Makampuni yaliyosajiliwa katika maeneo hayo imeongezeka  kutoka 44 mwaka 2010/2011 hadi 54 mwaka 2011/2012. Uwekezaji wa Mitaji umeongezeka kutoka Shilingi Trilioni 1.02 hadi Trilioni 1.1. Pia, mauzo ya Nje yameongezeka kutoka Shilingi Bilioni 560.5 hadi Bilioni 706.5 na  Ajira zimeongezeka kutoka 13,500 hadi 15,100.

47.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2012/2013, Serikali itaimarisha Sekta ya Viwanda kwa kuhimiza uwekezaji katika Viwanda vya kuongeza thamani ya mazao na bidhaa za kilimo na kuwaunganisha Wakulima na wenye Viwanda ili kuwawezesha kupata Soko la uhakika.  Aidha, itaendelea kuweka umuhimu katika utekelezaji wa miradi ya Makaa ya Mawe ya Mchuchuma na Chuma cha Liganga.

 

Madini


48.         Mheshimiwa Spika, Serikali imechukua hatua mbalimbali zenye lengo la kuboresha Sekta ya Madini ili Taifa linufaike zaidi na Rasilimali hiyo. Hatua hizo ni pamoja na kuimarisha Shirika la Madini la Taifa - STAMICO ili liweze kuchukua Hisa kwa niaba ya Serikali katika Migodi Mipya inayotarajiwa kuanzishwa. Kupitia utaratibu huo, STAMICO inamiliki  Asilimia 45 ya hisa katika Mgodi wa Backreef na Asilimia 55 zinamilikiwa na Mwekezaji. Hatua nyingine ni  kuwawezesha Wachimbaji Wadogo kuanzisha Vituo vya kuwasaidia kukopeshwa na kununua Vifaa vya Kisasa vya kuchimbia Madini katika maeneo ya Rwamgasa - Geita, Londoni – Manyoni na Pongwe – Bagamoyo. Aidha,  kupitia Wakala wa Ukaguzi wa Madini Nchini, shughuli za Ukaguzi katika Migodi mikubwa zimeimarishwa na sasa Migodi mingi imeanza kulipa Kodi ya Mapato.

49.         Mheshimiwa Spika, Serikali pia imechukua hatua madhubuti kuhakikisha kwamba Makampuni yote Makubwa ya Madini yanalipa mrabaha wa Asilimia Nne (4) kwa kuzingatia matakwa ya Sheria Mpya ya Madini Na. 14 ya mwaka 2010. Makampuni ya madini ambayo hayajazingatia matakwa haya ya Kisheria yametakiwa kulipa malimbikizo yote tangu Sheria hiyo ilipopitishwa mwaka 2010. Napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba, hakuna Kampuni ya Madini ambayo itakwepa kulipa Mrabaha kwa Kiwango kipya na Kodi zote kama inavyotakiwa. Tutakuwa makini kuhakikisha kwamba Sheria na Taratibu za Biashara ya Madini na Hifadhi ya Mazingira zinafuatwa na kila Mmiliki wa Mgodi. Napenda kutoa wito kwa  Wachimbaji Wadogo, jamii inayozunguka Migodi Mikubwa pamoja na wamiliki wa Migodi mikubwa kushirikiana kwa karibu na kila mmoja atimize wajibu wake ili kuleta mahusiano mazuri na kuepusha migogoro isiyokuwa ya lazima.

Utalii


50.         Mheshimiwa Spika, kutokana na juhudi zinazoendelea za kutangaza Vivutio mbalimbali vya Utalii, idadi ya Watalii imeongezeka kutoka 782,699 mwaka 2010 hadi 867,994 mwaka 2011, sawa na ongezeko la Asilimia 11.  Mapato yatokanayo na Utalii yameliingizia Taifa Shilingi Trilioni 2.14 mwaka 2011 ikilinganishwa na Shilingi Trilioni 1.96 mwaka 2010. Serikali pia, imeandaa Programu ya Kutunza na Kuweka Kumbukumbu za Urithi wa Malikale ili kupanua wigo wa Vivutio vya Utalii. Hatua hii itaiwezesha Tanzania kutangaza zaidi maeneo ya urithi wa Utamaduni wetu pamoja na Maeneo 22 ya Wapigania Uhuru kwa ajili ya Ukombozi wa Bara la Afrika. Katika mwaka 2012/2013, Serikali itaongeza kasi zaidi ya kutangaza Vivutio vya Utalii wetu nje ya Nchi, kwa kutumia Balozi zetu pamoja na Tovuti; kuwavutia Wawekezaji wa Nje na Ndani katika Sekta ya Utalii na kuhamasisha Utalii wa Ndani.

 

AJIRA


51.         Mheshimiwa Spika, Vijana ndiyo sehemu kubwa ya nguvu kazi katika Nchi yetu. Inakadiriwa kuwa Asilimia 35 ya Watanzania wote ni Vijana wenye umri kati ya miaka 15 hadi 35. Aidha, Vijana ni Asilimia 68 ya Watanzania wote wenye nguvu na uwezo wa kufanya kazi. Jitihada kubwa za Serikali zinaendelea kuwekwa katika kutoa msukumo kwenye uwekezaji katika sekta zenye fursa kubwa ya kutoa ajira  nyingi  kama  vile  kilimo, mifugo, uvuvi, ufugaji  nyuki, ujenzi, mawasiliano, uchukuzi, utalii na viwanda. Aidha, ili kuwawezesha Vijana kupata mitaji, Serikali imeongeza mtaji kwa Benki ya Rasilimali, Benki ya Wanawake, Benki ya Posta pamoja na Mifuko mbalimbali ya Uwezeshaji wananchi Kiuchumi. Vilevile, Mafunzo ya Ujasiriamali na  Elimu ya Ufundi Stadi kwa Vijana waishio Mijini na Vijijini yataimarishwa kwa lengo la kuwaongezea sifa katika Soko la Ajira, hasa Sekta Binafsi.

52.         Mheshimiwa Spika, ufumbuzi  wa uhakika wa tatizo la Ajira hususan kwa Vijana utatokana na jitihada za makusudi za kuongeza uwekezaji katika sekta zote. Napenda kutoa rai kwa Viongozi na Watendaji wote kwenye ngazi ya Taifa, Mikoa, Wilaya na Mamlaka za Serikali za Mitaa; kuhakikisha kwamba wanaongeza jitihada za kuboresha mazingira ya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji na kuongeza kasi ya ukuaji wa Sekta Binafsi.

HUDUMA ZA KIUCHUMI


Ardhi


53.         Mheshimiwa Spika, Ardhi ni Rasilimali muhimu katika Kukuza Uchumi na Kuondoa Umaskini. Hata hivyo, ili kunufaika na Rasilimali hiyo, ni muhimu Ardhi ipimwe na kuwa na Mpango endelevu wa matumizi bora ya Ardhi. Kwa kuzingatia umuhimu huo, hadi kufikia Aprili  2012, mipaka ya Vijiji 11,261 ilipimwa. Vyeti vya Ardhi ya Vijiji 3,283 vilitolewa, upimaji wa Viwanja 26,788 na Mashamba 706 ulifanyika na Hati za Hakimiliki za Kimila 46,063 zilitolewa na kufanya jumla ya Hati za Hakimiliki za Kimila zilizokwishatolewa Nchini kote kufikia 157,968.

54.         Mheshimiwa Spika, ili kuwawezesha Wananchi kunufaika na Rasilimali Ardhi wanayomiliki,  Serikali itakamilisha  Mradi wa Kuweka Kituo cha Kupokea Picha za  Satellite (Direct Satellite Imagery Receiving Station). Kituo hicho kitawawezesha Wananchi kupimiwa ardhi yao na kupatiwa hati kwa vile upimaji na utayarishaji wa ramani kwa ardhi yote Nchini utakuwa umerahisishwa kwa kiasi kikubwa. Huu utakuwa ukombozi wa kiuchumi kwa Watanzania.

55.         Mheshimiwa Spika, Serikali imekamilisha kujenga Mtandao Mpya wa Alama za Msingi za Upimaji Ardhi Nchini (National Geodetic Control Unit). Alama hizo zinatarajiwa kuanza kutumika mwezi Julai, 2012.  Mtandao wa Alama hizo, utarahisisha Upimaji wa Ardhi kwa matumizi mbalimbali na kupunguza gharama za upimaji Nchini.

Nishati


56.         Mheshimiwa Spika, mwezi Agosti 2011, Serikali iliwasilisha Bungeni Mpango wa Dharura wa Kuondoa Mgao wa Umeme uliokuwepo Nchini. Mgao huo ulisababishwa kwa kiasi kikubwa na kupungua kwa uzalishaji hasa kwenye Vyanzo vya Umeme vya Maji.  Kutokana na utekelezaji wa Mpango wa Dharura wa Umeme hadi kufikia mwezi Aprili 2012, jumla ya Megawati 342 zimezalishwa na kuingizwa kwenye Gridi ya Taifa. Uzalishaji huo umeimarisha hali ya upatikanaji Umeme na hivyo Makali ya Mgao kupungua. Hata hivyo, uzalishaji wa Umeme wa Dharura ni wa gharama kubwa kutokana na Mitambo mingi kuendeshwa kwa kutumia Mafuta ya Dizeli.

57.         Mheshimiwa Spika, hatuwezi kuendelea na hali hii ya uzalishaji umeme kwa gharama kubwa huku tukiwa na Rasilimali zinazoweza kubadili kabisa hali hiyo. Kwa hiyo, Serikali imeanza kutekeleza Mradi mkubwa wa ujenzi wa Bomba la Gesi kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam kwa lengo la kuongeza kiasi cha Gesi itakayotumika kuendesha Mitambo ya Uzalishaji Umeme. Tayari fedha za kutekeleza mradi huu zimepatikana na ujenzi unatarajiwa kuanza mwaka 2012/2013. Serikali pia katika mwaka 2011/2012 imetoa Shilingi Bilioni 39 ikiwa ni sehemu ya mchango wake katika ujenzi wa Mradi huo. Fedha nyingine kiasi cha Shilingi Bilioni 110 zimewekwa katika Bajeti ya 2012/2013.

58.         Mheshimiwa Spika, hatua nyingine ambayo Serikali imechukua kutatua tatizo la Umeme Nchini ni kuongeza ushiriki wa Sekta Binafsi katika uzalishaji na usafirishaji wa umeme. Kwa kuanzia, Serikali inashirikiana na Serikali ya Marekani kubaini vikwazo vinavyozuia Sekta Binafsi kuwekeza kwenye Miradi mikubwa ya Umeme. Kazi hiyo itafuatiwa na utekelezaji wa Mpango Maalum wa Pamoja wa Miaka Mitano utakaoanza kutekelezwa mwaka 2012/2013. Lengo ni Kuzalisha Umeme wa MW 2,700 ifikapo mwaka 2016.

59.         Mheshimiwa Spika, Wakala wa Umeme Vijijini unatekeleza Programu Kabambe ya Kusambaza Umeme Vijijini katika Mikoa 16. Mikoa hiyo ni Kigoma, Kagera, Mwanza, Mara, Shinyanga, Arusha, Kilimanjaro, Manyara, Tanga, Pwani, Morogoro, Dodoma, Singida, Mbeya, Rukwa na Tabora. Chini ya Programu hiyo, Miradi Midogo 41 inatekelezwa ambapo Wateja 22,000 watalipiwa gharama za kuunganisha Umeme kupitia Mfuko wa Nishati Vijijini. Programu hiyo itawawezesha Wananchi wengi zaidi Vijijini kupata Nishati ya Umeme ili kuharakisha maendeleo katika maeneo hayo.

 

60.         Mheshimiwa Spika, kutokana na jitihada za Serikali za kuvutia uwekezaji katika Sekta ya Nishati, kasi ya utafutaji na ugunduzi wa hazina mpya ya Gesi Asili Nchini imeongezeka. Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba, hivi karibuni Makampuni yanayofanya utafiti wa Gesi Asili Nchini yamegundua kiasi kikubwa cha Gesi Asili yenye futi za ujazo Trilioni 3. Gesi hiyo imegundulika kwenye kina cha maji marefu baharini takriban Kilometa 80 kutoka Nchi kavu Mashariki mwa Mkoa wa Lindi. Ugunduzi huo unafanya kiasi cha Gesi kilichogundulika hadi sasa kwenye kina cha maji marefu baharini kufikia futi za ujazo Trilioni 20.97. Kwa kuzingatia fursa zinazotokana na kasi kubwa ya ukuaji wa Sekta ya Gesi Nchini, Serikali imejipanga kuhakikisha kwamba Taifa linanufaika kikamilifu na ugunduzi wa rasilimali hiyo. Serikali inaandaa Sera na Sheria Mahsusi ya Gesi Asili pamoja na Mpango Kabambe wa Matumizi ya Gesi kwa lengo la kuimarisha usimamizi na uendelezaji wa sekta hiyo. Aidha, Serikali itawawezesha Vijana wetu kupata Mafunzo Maalum (Specialized Training) yanayohusiana na masuala ya Gesi Asili kwa lengo la kupata Wataalam Wazalendo waliobobea kwenye sekta hii kama ilivyoainishwa kwenye Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano. 

Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA)


61.         Mheshimiwa Spika, Nchi zote Duniani zimeazimia kubadili Teknolojia ya Utangazaji kutoka Analojia kwenda Dijitali ambayo imeonekana kuwa na tija na yenye kutumiwa na Vifaa vingi zaidi vya Mawasiliano. Kwa kuzingatia azimio hilo, Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki nazo zimekubaliana kutekeleza mabadiliko hayo na kuanza Kurusha Matangazo katika Mfumo wa Dijitali pekee ifikapo tarehe 31 Desemba 2012. Ili Watanzania wawe tayari kuyapokea mabadiliko hayo, Serikali imeandaa mpango wa kuelimisha Umma unaojulikana kwa jina la “Digital Tanzania” ambao ulizinduliwa rasmi na Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mwezi Agosti 2011. Wananchi wote watambue kwamba mabadiliko ya Teknolojia za Utangazaji kutoka Analojia kwenda Dijitali ni matokeo ya ukuaji wa kasi wa Teknolojia ya Mawasiliano ambao hatuwezi kuuepuka.

62.         Mheshimiwa Spika,  katika mwaka 2011/2012, Awamu ya Pili ya Ujenzi wa Mkongo wa Mawasiliano wa Taifa wenye urefu wa Kilomita 3,000 umekamilika na kuanza kutumika. Kukamilika kwa Awamu hii kunafanya Nchi yetu kuwa na Mkongo uliojengwa wenye jumla ya Kilometa  7,300  na  kumeiwezesha Mikoa yote ya Tanzania Bara kuunganishwa kwenye Mkongo huo. Aidha, Mkongo wa Mawasiliano wa Taifa umeunganishwa na Kisiwa cha Pemba kupitia Tanga. Katika mwaka 2012/2013, Kisiwa cha Unguja kitaunganishwa na Mkongo huo kupitia Dar es Salaam, baada ya kukamilika kwa ujenzi wa Mkongo wa Majini.

Barabara na Madaraja


63.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/2012, Serikali imeendelea kujenga, kukarabati na kuzifanyia matengenezo Barabara Kuu, za Mikoa na Wilaya ili ziweze kupitika wakati wote.  Hadi mwezi Mei 2012, Serikali imejenga jumla ya Kilometa 305.6 za Barabara Kuu na Kilometa 29.5 za Barabara za Mikoa kwa kiwango cha Lami.  Pia, imefanya ukarabati mkubwa wa Kilometa 78.4 za Barabara Kuu kwa kiwango cha Lami na Kilometa 463.2 kwa kiwango cha Changarawe katika Barabara za Mikoa.  Aidha, jumla ya Kilometa 7,209 za Barabara za Mamlaka ya Serikali za Mitaa zimefanyiwa matengenezo ya kawaida. Vilevile, ujenzi wa Daraja la Nangoo lililopo Mtwara na Daraja la Malagarasi Mkoani Kigoma umeanza.

64.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2012/2013, Serikali imepanga kujenga Kilometa 414 na kukarabati Kilometa 135 kwa kiwango cha Lami pamoja na kujenga Madaraja 11 katika Barabara Kuu. Vilevile, itajenga Kilometa 573 kwa kiwango cha Changarawe na Kilometa 32 kiwango cha Lami katika Barabara za Mikoa pamoja na Madaraja 27.  Katika kipindi hicho, Mfuko wa Barabara unatarajiwa kuingiza zaidi ya Shilingi Bilioni 400 ambazo zitatumika kwa ajili ya matengenezo, ujenzi na usimamizi wa Miradi mbalimbali ya Barabara, zinazosimamiwa na TANROADS na Mamlaka za Serikali za Mitaa.

 

Bandari


65.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/2012, Serikali imeendelea kuboresha miundombinu na kuongeza ufanisi wa utoaji huduma katika Bandari Kuu za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara pamoja na kukarabati Bandari za Kigoma na Mwanza. Aidha, imekamilisha Upembuzi Yakinifu wa ujenzi wa Bandari Mpya ya Mbegani (Bagamoyo) na Mwambani Tanga.

Reli


66.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/2012, Serikali iliweka Menejimenti Mpya ya Shirika la Reli (TRL) inayoongozwa na Wazalendo. Serikali pia ilitoa fedha za kukarabati Miundombinu chakavu ya Reli ya Kati ikiwa ni pamoja na ukarabati wa Injini za Treni na Mabehewa ya Abiria. Aidha, kazi ya usanifu wa kina kwa ajili ya kuijenga Reli ya Kati kwa kiwango cha Kimataifa (Standard Gauge) na kuiunganisha na Nchi za Rwanda na Burundi imeanza mwezi Februari 2012 na inatarajiwa kukamilika Mwaka 2013.

67.         Mheshimiwa Spika, Serikali za Tanzania, Zambia na Jamhuri ya Watu wa China mwezi Machi 2012, zimesaini Mikataba yenye Thamani ya Shilingi Bilioni 66.67 kwa ajili ya kuboresha Miundombinu na huduma za TAZARA. Mikataba hiyo itatekelezwa kuanzia mwaka 2012/2013. Jitihada hizo zitawezesha huduma za Reli kuimarika na hivyo kutoa mchango mkubwa katika uchumi wetu.

 


HUDUMA ZA JAMII


Elimu


Elimu ya Msingi


68.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/2012, Serikali imeanza kufanya Mapitio ya Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 1995 kwa lengo la kuiboresha ili kuendana na Mazingira ya sasa.  Kazi hiyo inatarajiwa kukamilika Mwaka 2012/2013. Aidha, Serikali iliendelea na Utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi ambapo jumla ya Madarasa 485 na Nyumba za Walimu 344 zilijengwa na Madawati 61,363 yalinunuliwa. Katika kipindi hicho, jumla ya Walimu 11,243 waliajiriwa na 2,259 walipewa mafunzo kazini ili kuongeza ubora wa ufundishaji wa Masomo ya Sayansi, Hisabati na Kiingereza. Lengo ni kuwajengea Walimu uwezo wa kufundisha na hatimaye kuongeza kiwango cha Ufaulu wa Wanafunzi katika masomo hayo.

Elimu ya Sekondari


69.         Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2011/2012, utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Mpango wa Elimu ya Sekondari (MMES II) umekuwa na mafanikio ya kuridhisha. Jumla ya Madarasa 1,316, Maabara 127 na Nyumba za Walimu 270 zilijengwa na Madawati 123,855 yalinunuliwa. Katika kipindi hicho, jumla ya Walimu wa Sekondari 13,900 wameajiriwa na Vitabu Milioni 1.5 vilinunuliwa na kusambazwa katika Shule mbalimbali za Sekondari. Wanafunzi waliojiunga na Kidato cha Kwanza waliongezeka kutoka 456,350 Mwaka 2011 hadi 517,993 Mwaka 2012. Hili ni ongezeko la Wanafunzi 61,643.

70.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2012/2013, Serikali itaendelea kuimarisha Miundombinu ya Shule za  Sekondari ili kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia. Jitihada zitaongezwa katika kuhamasisha ujenzi wa Madarasa zaidi kwa ajili ya Wanafunzi wanaojiunga na Kidato cha Tano na Sita kukidhi mahitaji makubwa yaliyojitokeza baada ya kupanuliwa kwa Elimu ya Sekondari Nchini.

Mafunzo ya Ufundi Stadi


71.         Mheshimiwa Spika, Mafunzo ya Ufundi Stadi yana mchango mkubwa katika kuwapatia ujuzi na kuwajengea uwezo Wanafunzi wanaohitimu Elimu ya Msingi na Sekondari. Katika mwaka 2011/2012, Serikali imekamilisha ujenzi  wa  Vyuo vya  Mafunzo ya Ufundi  Stadi  katika Mikoa ya Lindi, Pwani, Manyara, Arusha na Dar es Salaam. Kukamilika kwa Vyuo hivyo kumeongeza idadi ya Wanafunzi wanaojiunga na Vyuo vya Ufundi kutoka 72,938 mwaka 2010 hadi 102,217 mwaka 2011. Katika Mwaka 2012/2013, Serikali itapanua zaidi Mafunzo ya Ufundi Stadi Nchini.

Elimu ya Juu


72.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/2012, Serikali ilitekeleza Mpango wake wa kuimarisha Miundombinu ya Vyuo Vikuu na Vyuo vya Elimu ya Juu Nchini.  Kutokana na hatua hiyo, Udahili wa Wanachuo katika Vyuo Vikuu na Vyuo Vikuu Vishiriki uliongezeka  kutoka Wanachuo 40,993 mwaka 2005/2006 hadi 139,638 mwaka 2010/2011. Idadi ya Wanachuo waliopewa mikopo ya elimu ya juu ikijumuisha Wanachuo wa Vyuo Vikuu na Vyuo vingine iliongezeka kutoka 42,729 mwaka 2005/2006 hadi 93,784 mwezi Aprili 2012. Aidha, katika kipindi hicho, fedha zilizokopeshwa Wanachuo hao ziliongezeka kutoka Shilingi Bilioni 56.1 hadi Bilioni 291.  Katika Mwaka 2012/2013, Serikali itatoa kipaumbele katika kuongeza ubora wa Elimu ya Juu ili kuendana na mahitaji ya Soko la Ajira Nchini na katika Jumuiya ya Afrika Mshariki.

Afya


73.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/2012, Serikali imetekeleza Mpango wa kugawa Vyandarua vyenye Dawa ili kupunguza Maambukizi ya Ugonjwa wa Malaria.  Hadi Desemba 2011 jumla ya Vyandarua Milioni 17.6 viligawanywa bila malipo kwa kila Kaya yenye Watoto wenye umri chini ya Miaka Mitano Nchi nzima. Sambamba na hatua hiyo, Mpango wa Kunyunyizia Dawa ya Ukoko aina ya ICON kwenye kuta za Nyumba ili kuua mbu ulitekelezwa katika Wilaya 18 za Mikoa ya Kagera, Mwanza na Mara ambayo imeonekana kuwa na Maambukizi makubwa ya Malaria. Aidha, jitihada za kuongeza upatikanaji wa Dawa Mseto za kutibu Malaria kwa bei yenye punguzo zinaendelea. Jitihada za udhibiti wa malaria zimechangia kupunguza vifo vya watoto wachanga kutoka vifo 99 kwa kila watoto 1,000 mwaka 1999 hadi vifo 51 kwa kila watoto 1,000 mwaka 2010. Vilevile, vifo vya watoto wa umri chini ya miaka mitano vimepungua kutoka vifo 147 kwa kila watoto 1,000 mwaka 1999 hadi vifo 81 kwa kila Watoto 1,000 mwaka 2010.

74.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2012/2013, Serikali itaendelea na utekelezaji wa Mpango wa Kuangamiza Viluwiluwi vya Mbu kwa kutumia njia za Kibaiolojia kwa ushirikiano na Serikali ya Cuba. Mpango huo ulianza mwaka 2011 kwa majaribio katika Jiji la Dar es Salaam. Aidha, Serikali itaandaa Mkakati Maalum wa kugawa Vyandarua kupitia Shuleni ili kuhakikisha kuwa matumizi ya Vyandarua yanakuwa endelevu. Natoa wito kwa Wananchi wote kutumia Vyandarua vinavyotolewa na Serikali kwa lengo lililokusudiwa badala ya matumizi mengine. Vilevile, nawahimiza kutokomeza Mazalia ya Mbu na kuweka Mazingira katika hali ya Usafi ili tufanikiwe kuondoa Ugonjwa wa Malaria Nchini.

75.         Mheshimiwa Spika, Serikali imedhamiria kupunguza idadi kubwa ya Wagonjwa wa Moyo wanaopoteza maisha kwa kukosa Tiba Stahiki na gharama kubwa inayotumika kupata Tiba hiyo nje ya Nchi. Ili kutekeleza dhamira hiyo, katika mwaka 2011/2012, Serikali kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China imekamilisha ujenzi wa Kituo cha Kisasa cha Upasuaji, Tiba na Mafunzo ya Ugonjwa wa Moyo katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Pamoja na mafanikio hayo, Hospitali ya Taifa ya Muhimbili iliendelea kutoa huduma za Upasuaji Mkubwa wa Moyo ambapo hadi mwezi Aprili, 2012 jumla ya Wagonjwa 300 walipata huduma hiyo na hivyo kuokoa zaidi ya Shilingi Bilioni Sita (6) ambazo zingetumika kuwapeleka Wagonjwa hao Nje ya Nchi. Napenda kuwapongeza Madaktari na Wahudumu wote wa Afya kwa huduma nzuri wanayotoa kwa  wagonjwa. Nawasihi kuendelea na moyo huo, kwani wamepewa dhamana kubwa ya kuwahudumia wananchi kutokana na ujuzi na weledi walionao.

Huduma kwa Watu wenye Ulemavu


76.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/2012, Serikali imekamilisha zoezi la kuandaa Kanuni za utekelezaji wa Sheria ya Watu wenye Ulemavu iliyopitishwa na Bunge mwaka 2010.  Utekelezaji wa Sheria hiyo umeanza ambapo Watu wenye Ulemavu wanapatiwa haki na huduma za msingi ikiwemo elimu, afya, ajira na kulindwa Kisheria. Kwa Watu wenye Ulemavu wa Ngozi, Serikali kwa kiasi kikubwa imedhibiti   Vitendo  vya  Ukatili  walivyokuwa  wanafanyiwa. Napenda kutumia fursa hii kutoa Wito kwa Wananchi wote kuwapenda na kuwahudumia Walemavu wakiwemo Watu wenye Ulemavu wa Ngozi.

 

Lishe


77.         Mheshimiwa Spika, katika Hotuba yangu ya Bajeti ya mwaka 2011/2012, nililitaarifu Bunge kuhusu hali isiyoridhisha ya Lishe hapa Nchini na hatua ambazo Serikali imeanza kuzichukua kukabiliana na hali hiyo. Napenda kulifahamisha   Bunge   lako   kuwa,  Mkakati  wa  Kitaifa  wa Lishe  ulizinduliwa  rasmi   tarehe   20  Septemba,  2011. Mkakati huo umeainisha maeneo ya kipaumbele ambayo yatatekelezwa katika kipindi cha Miaka Mitano ili kupunguza idadi ya Watoto wenye Uzito Pungufu, Udumavu, pamoja na idadi ya Wanawake Wajawazito wenye Upungufu wa Damu. 

78.         Mheshimiwa Spika, ili kuliongezea uzito suala la Lishe, Kamati zitakazohakikisha kwamba Mkakati wa Lishe  unatekelezeka  kikamilifu  zimeanzishwa katika ngazi ya Taifa na Halmashauri. Napenda kutoa msisitizo wa kipekee kwamba Lishe Bora ni muhimu kwa maendeleo  ya  Watu  na  Taifa  kwa ujumla.  Lishe Duni ina  Madhara makubwa hasa kwa Watoto wadogo; Mtoto mdogo anapokosa Lishe Bora, maendeleo yake katika masomo yana walakini mkubwa na hali hiyo haiwezi kurejeshwa tena. Hivyo, Watendaji katika ngazi zote watoe umuhimu mkubwa kwenye suala la Lishe Bora kwa kuendelea kutoa elimu ya Lishe Bora ili Wananchi walielewe na wale chakula chenye Virutubisho muhimu ambavyo vipo kwenye maeneo mengi Nchini. 

Maji


79.         Mheshimiwa  Spika,  Serikali  imeboresha  huduma ya maji Vijijini kwa kujenga Miradi mipya, kupanua na kukarabati iliyopo kwa kushirikisha Wananchi. Katika mwaka 2011/2012,  Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW) iliendelea na utekelezaji wa mradi wa maji katika Wilaya za Moshi Vijijini na Hai. Vilevile, kwa kushirikiana na Serikali ya Japan iliendelea kutekeleza mradi wa maji Vijijini katika Mikoa ya Mwanza, Mara na Tabora. Aidha,  Serikali imeendelea na juhudi zake za kujenga mabwawa ya maji katika maeneo kame Nchini. Mabwawa yanayoendelea kujengwa ni Kawa (Nkasi), Sasajila (Chamwino), Matwiga (Chunya), Nyambori (Rorya), Wegero (Musoma), Habiya (Bariadi), Iguluba (Iringa), Mwanjoro (Meatu) na Seke Ididi (Kishapu).

80.         Mheshimwa Spika, Serikali pia, imeimarisha usimamizi na uendelezaji wa Rasilimali za Maji katika Mabonde yote Tisa (9) ya Maji Nchini na kutoa elimu kuhusu umuhimu wa Kutunza Vyanzo vya Maji katika Mamlaka za Serikali za Mitaa. Aidha, Serikali imejenga Visima 946 katika Halmashauri 84.

81.         Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Mijini, Serikali imejenga na kukarabati Mifumo ya Maji katika Miji Mikuu ya Mikoa 19. Kutokana na jitihada hizo, kiwango cha upatikanaji wa Maji kwa wakazi wa Miji hiyo kimeongezeka kutoka Asilimia 84 mwaka 2010 hadi kufikia Asilimia 86 mwaka 2011. Katika mwaka 2012/2013, Serikali itaendelea kuboresha upatikanaji wa Maji Mijini kwa kuimarisha utendaji wa Mamlaka za Maji za Miji Nchini. Kwa upande wa Jiji la Dar es Salaam, Serikali itakamilisha upanuzi wa Mtambo wa Ruvu Chini na kuanza ujenzi wa Bomba Jipya la Maji kutoka Ruvu Chini hadi kwenye Matenki ya Maji yaliyopo maeneo ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Aidha, itakamilisha Usanifu wa Mradi wa Kuchimba Visima Virefu katika maeneo ya Kimbiji na Mpera na kuanza ujenzi wa Visima hivyo.

ULINZI NA USALAMA


82.         Mheshimiwa Spika, Majeshi yetu ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa yanafanya kazi nzuri kuhakikisha kwamba hali ya Usalama wa Nchi na Mipaka yetu ni shwari. Aidha, Majeshi yetu yameshiriki kikamilifu katika shughuli za kiraia kusaidia Wananchi wakati wa Majanga hususan mafuriko, ajali na milipuko ya magonjwa. Pamoja na kazi hizo, katika mwaka wa 2011/2012, Jeshi la Kujenga Taifa limekamilisha ukarabati wa Makambi 10 ya Jeshi la Kujenga Taifa yenye uwezo wa kuchukua Vijana 20,000 kwa wakati mmoja. Kwa mwaka 2012/2013, jumla ya Vijana 5,000 wataanza tena kujiunga na JKT kwa Mujibu wa Sheria.

83.         Mheshimiwa Spika, katika kuitikia Wito wa kutekeleza Azma ya KILIMO KWANZA, mwaka 2011/2012, Jeshi la Kujenga Taifa limezalisha Tani 731.5 za mbegu bora zenye thamani ya Shilingi Milioni 544.4. Katika mwaka 2012/2013, Serikali itaendelea kuyawezesha Majeshi yetu kwa Vifaa na Zana za Kivita na upatikanaji wa mahitaji muhimu. Serikali pia itaendelea kukarabati Makambi ya Jeshi la Kujenga Taifa kwa ajili ya kuchukua Vijana wengi zaidi na pia kujenga maghala salama ya kuhifadhia silaha, mabomu na milipuko.

84.         Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge watakubaliana na mimi kwamba Jeshi la Polisi linafanya kazi kubwa ya kudhibiti Matukio ya Uhalifu hapa Nchini. Mafanikio hayo yamepatikana kutokana na ushirikiano mzuri kati ya Polisi na Wananchi kupitia Mkakati wa Ulinzi Shirikishi. Moja ya Mbinu zinazotumika na Jeshi hilo ni kuwashirikisha Wadau, hasa Viongozi wa Kijamii kama vile Wazee wa Kimila, Madhehebu ya Dini, Vyama vya Hiari katika kuhamasisha Wananchi kuzuia na kudhibiti Uhalifu Nchini. Mbinu nyingine ni kudhibiti tatizo la kuzagaa kwa Silaha Ndogo Nchini kwa Kusajili na kuhamasisha Wananchi kujitokeza kuwekewa Alama Maalum kwenye Silaha wanazomiliki. Hadi kufikia mwezi Februari 2012, jumla ya Silaha Ndogo 1,250 zilisajiliwa. Natumia fursa hii kuvipongeza Vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama kwa kazi nzuri wanayofanya kuhakikisha Nchi yetu inakuwa salama.

85.         Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio hayo, tunayo changamoto ya Ajali nyingi za Barabarani. Ajali hizo zimeendelea kupoteza maisha ya Watu wengi na kusababisha Ulemavu wa Kudumu kwa wengine. Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na Wadau wengine lijipange kukabiliana na Ajali hizo kwa umakini ili kuokoa maisha ya Watanzania yanayopotea kutokana na Ajali ambazo zinazuilika. Hii ni pamoja na kuendelea kutoa elimu ya Usalama Barabarani; kufanya ukaguzi wa mara kwa mara; kuwachukulia hatua za Kisheria Madereva Wazembe na kuweka Mfumo madhubuti wa kudhibiti Mwendo Kasi wa Magari.

USHIRIKIANO WA KIMATAIFA NA KIKANDA


86.         Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza Sera ya Diplomasia ya Uchumi inayoweka umuhimu katika ushirikiano wenye maslahi ya kiuchumi kwa Nchi yetu na Nchi nyingine pamoja na Mashirika ya Kimataifa. Tayari tumeanza kushuhudia mafanikio ya Sera hii kutokana na kazi nzuri inayofanywa na Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Balozi zetu kwa kudumisha mahusiano mema na kuitangaza Tanzania katika medani za Kimataifa. Jitihada hizo, zimewezesha kuvutia Wawekezaji wengi, kuongeza idadi ya Watalii, fursa za kibiashara na ajira.  

87.         Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha Mtangamano wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki Nchi Wanachama zinatekeleza makubaliano ya kuanzisha Vituo vya Utoaji Huduma kwa Pamoja Mipakani (One Stop Boarder Posts). Hadi sasa ujenzi wa Vituo Vinne vya Mpakani vya Horohoro, Holili,  Sirari  na  Mtukula  uko  katika  hatua  za  kukamilika.

Pamoja na hatua hizo, mwenendo wa biashara baina ya Tanzania na Jumuiya Afrika ya Mashariki umezidi kuimarika ambapo mauzo nje yameongezeka kwa Asilimia 12.8 kutoka Shilingi Bilioni 512.76 mwaka 2010 hadi Shilingi Bilioni 578.39 mwaka 2011. Serikali inaendelea na maandalizi ya Sera ya Mtangamano ambayo itakuwa mwongozo wa utekelezaji wa shughuli za Kitaifa za Mtangamano wa Kikanda na Mkakati wa Utekelezaji wa Soko la Pamoja.

TAWALA ZA MIKOA NA MAMLAKA ZA SERIKALI ZA MITAA

 

88.         Mheshimiwa Spika, mwaka 2010/2011, Serikali ilitangaza nia ya kuanzisha maeneo Mapya ya Utawala ya Mikoa minne ya Simiyu, Katavi, Njombe na Geita pamoja na Wilaya Mpya 19 na Tarafa 34 kwa lengo la kusogeza na kurahisisha utoaji wa huduma kwa Wananchi. Tayari Serikali imeyaanzisha rasmi Maeneo hayo na Uteuzi wa Viongozi wa kusimamia Mikoa na Wilaya hizo umefanywa.

89.         Mheshimiwa Spika, ili kuwezesha Viongozi wa Mikoa na Wilaya kutekeleza majukumu yao ipasavyo, Serikali imetoa Mafunzo kwa Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya zote Nchini mwezi Mei, 2012. Aidha, Serikali imetekeleza ahadi yake ya kutoa Mafunzo kwa Madiwani 4,451 Nchini. Ni imani yangu kwamba baada ya mafunzo hayo, utendaji kazi wa Viongozi hao utakuwa ni wa ufanisi zaidi.

90.         Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kusogeza huduma kwa Wananchi kwa kuzipandisha hadhi Mamlaka za  Serikali  za  Mitaa.  Mamlaka  za  Miji  Midogo ya Geita, Bariadi na Tarime zimepandishwa hadhi na kuwa Halmashauri za Miji.  Vilevile, Tangazo la kuanzishwa kwa Halmashauri za Manispaa za Lindi na Ilemela limetolewa kwenye Gazeti la Serikali Na.182 na 256, na Tangazo la Kupandishwa Hadhi kwa Halmashauri ya Manispaa ya Arusha kuwa Halmashauri ya Jiji limetolewa katika Gazeti la Serikali Na. 341. Serikali inaendelea na taratibu za kuanzisha Halmashauri za Wilaya 25 Mpya zikiwemo 19 kwenye Wilaya Mpya zilizoanzishwa na sita kutokana na kugawa baadhi ya Halmashauri.

91.         Mheshimiwa Spika, itakumbukwa kuwa wakati nahitimisha mjadala wa Hotuba ya Bajeti ya Ofisi yangu mwaka jana, niliahidi kuwa Serikali itaangalia upya viwango vya Posho za Waheshimiwa Madiwani kwa lengo la kuviongeza. Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba zoezi hilo limekamilika na kuanzia mwaka 2012/2013 Waheshimiwa Madiwani watalipwa Viwango Vipya vya Posho vilivyoboreshwa.

 

MASUALA MTAMBUKA


Jinsia


92.         Mheshimiwa Spika, Ibara ya 176 ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2010, inahimiza kutambua uwezo na nguvu kubwa ya Wanawake katika kusukuma kasi ya maendeleo na kuleta mageuzi ya Kiuchumi, Kijamii na Kisiasa. Katika mwaka 2011/2012, Serikali imeandaa Mkakati na Mwongozo wa Kitaifa wa Kuzuia Ukatili wa Kijinsia Nchini. Aidha, imeunda na kuzindua  Kamati  ya Kitaifa ya Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto. Katika mwaka 2012/2013, Serikali itaendelea kutoa fursa zaidi za kuwawezesha Wanawake katika Nyanja mbalimbali pamoja na kuratibu Utekelezaji wa Mikataba ya Kikanda na Kimataifa kuhusu Haki za Wanawake na Watoto.

 

Vita Dhidi ya Rushwa


93.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/2012, Serikali imeendelea na Mapambano Dhidi ya Vitendo vya Rushwa Nchini. Jumla ya Tuhuma zilizopokelewa hadi Mei 2012 ni 4,498. Kati ya hizo, Tuhuma 884 uchunguzi wake umekamilika na majalada yamefunguliwa. Aidha, Kesi 612 ziliendeshwa Mahakamani; na Kati ya hizo, Kesi 478 zinaendelea na 134 zilitolewa uamuzi  ambapo Kesi 46 watuhumiwa walipatikana na hatia na kuadhibiwa, Kesi 32 ziliondolewa Mahakamani kutokana na sababu mbalimbali na  Kesi 56 watuhumiwa wake waliachiwa huru. Vilevile, Mafunzo kuhusu Vita Dhidi ya Rushwa yametolewa kwa Wanajamii 328,947 na Watumishi 439 wa Serikali. Katika mwaka 2012/2013, Serikali itaendelea kuchunguza Tuhuma 2,729 zilizopo na Tuhuma mpya zitakazopokelewa pamoja na kuendelea na Uchunguzi Maalum wa Tuhuma zilizobainishwa kwenye Taarifa za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali kuhusu Ubadhirifu katika Taasisi mbalimbali za Serikali.

Mazingira


94.         Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutekeleza Sera, Mikakati, Sheria, Kanuni na Miongozo ya Kuhifadhi Mazingira. Miongoni mwa kazi zilizotekelezwa ni pamoja na kuandaa Kanuni 14 za Usimamizi wa Mazingira ikiwemo Udhibiti wa Taka, Matumizi ya Bioteknolojia ya Kisasa na tathmini na ukaguzi wa athari za Mazingira. Pamoja na miongozo hiyo, Miradi 130 imefanyiwa tathmini na kupatiwa Hati za Tathmini ya Athari kwa Mazingira, Kampeni ya Upandaji Miti imeendeshwa na mafunzo kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi yametolewa. Serikali itaendelea kuzijengea uwezo Mamlaka za Serikali za Mitaa kutekeleza Mikakati ya Kuhifadhi Mazingira kwa kushirikiana na Wadau wengine. Serikali pia itaendelea kutekeleza Mpango wa Kitaifa wa Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi, kutoa Elimu ya Hifadhi ya Mazingira kwa Umma na kuhamasisha utekelezaji wa Kampeni ya Upandaji Miti Nchini.

 

Maafa


95.         Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/2012, Serikali imeshughulikia matukio ya Maafa katika maeneo mbalimbali Nchini. Maafa hayo yalisababishwa na mafuriko, magonjwa ya  mlipuko,  upepo  mkali   na  ukame  uliosababisha baadhi  ya  maeneo  kupata  upungufu  wa chakula. Ukame ulizikumba Wilaya 55 na kuathiri Watu 2,186,990 ambao walihitaji msaada wa chakula. Hadi mwezi Mei 2012, Serikali imetoa Tani 69,688 zenye thamani ya Shilingi Bilioni 24.4 kwa waathirika ikiwa ni chakula cha msaada. Vilevile, imetoa Shilingi Bilioni 5.5 kwa ajili ya kusafirishia chakula hicho hadi kwa walengwa. 

96.         Mheshimiwa Spika, Serikali pia iliendelea kushughulikia Waathirika wa Milipuko ya Mabomu iliyotokea tarehe 16 Februari 2011, katika Kambi ya Jeshi  ya Gongo la Mboto, Dar-es-Salaam. Serikali inakamilisha ujenzi wa Nyumba 36 za Waathirika wa Mabomu zilizobomoka kabisa ambazo zinajengwa na SUMA JKT katika eneo la Msongola, Manispaa ya Ilala.

97.         Mheshimiwa Spika, Mafuriko yaliyotokea Jijini Dar es Salaam mwezi Desemba 2011, yalikuwa na athari kubwa. Mafuriko hayo, yalisababisha Watu 41 kupoteza maisha,  mali nyingi za Wananchi kupotea na miundombinu ya barabara, madaraja, umeme na maji kuharibika. Serikali kwa kushirikiana na Wadau mbalimbali ilichukua hatua za kuwasaidia waathirika wa mafuriko kwa kuwapatia misaada ya kibinadamu kama vile, makazi ya muda, chakula, mavazi, malazi na huduma za matibabu. Serikali pia imewapatia waathirika waliokuwa wamejenga nyumba zao mabondeni viwanja katika eneo la Ekari 360 lililopo Mabwepande, Wilayani   Kinondoni   ili   waweze   kujenga  makazi  mapya. Hadi mwezi Mei 2012,  Kaya 1,010 zilizoainishwa kuwa katika maeneo hatarishi zaidi zimetengewa viwanja. Vilevile, miundombinu muhimu katika eneo hilo ikiwemo maji, barabara na umeme pamoja na huduma za afya, elimu na Kituo cha Polisi imejengwa.

98.         Mheshimiwa Spika, ili kuondoa tatizo la Wananchi kujenga katika maeneo Hatarishi, Serikali imeziagiza  Mamlaka za Serikali za Mitaa Nchini ziandae Mipango endelevu ya kuwaondoa Watu wanaoishi mabondeni na kuwahamishia katika maeneo salama.  Halmashauri za Jiji la Dar es Salaam tayari zimeandaa Mpango ambao utaanza kutekelezwa katika Bajeti ya mwaka 2012/2013.

99.         Mheshimiwa Spika, mwaka jana, wakati nahitimisha Hotuba ya Makadirio ya Ofisi yangu, niliahidi kuwa Serikali itatoa Kifuta Machozi kwa Wafugaji ambao Mifugo yao ilikufa kutokana na Ukame Mkali uliotokea mwaka 2008/2009. Athari za Ukame huo, ni pamoja na Vifo vingi vya Mifugo, zikiwemo Ng’ombe, Mbuzi na Kondoo katika Wilaya za Monduli, Longido na Ngorongoro. Kutokana na hali hiyo, mfumo wa maisha wa Wafugaji wengi ulivurugika kwa kuwa Uchumi wao unategemea zaidi Ufugaji. Baada ya tathmini kufanyika, Serikali iliamua kutoa mifugo ya kianzio (seed stock) ili  kuziwezesha  Kaya  zilizopoteza  Mifugo  yote kuendeleza  ufugaji. Utekelezaji  wa zoezi hilo umeanza na  utaendelea  katika  kipindi  cha  mwaka  ujao  wa fedha. Napenda kutumia fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uamuzi wake wa busara wa kuwawezesha Wafugaji hao na kushiriki yeye binafsi katika uzinduzi wa Mpango huo uliofanyika tarehe 19 Februari 2012, Wilayani Longido.

100.      Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2012/2013, Serikali itajenga uwezo zaidi wa Nchi yetu wa Kuzuia, Kujiandaa na Kukabiliana na Maafa na kurejesha hali ya kawaida kwa Waathirika. Aidha, Serikali itakamilisha maandalizi ya Sheria Mpya ya Menejimenti ya Maafa, mapitio ya Sera ya Menejimenti ya Maafa ya mwaka 2004 na Mpango Mkakati wa Utekelezaji wa Sera hiyo.

Udhibiti wa UKIMWI


101.      Mheshimiwa Spika, Tanzania  ni moja kati ya Nchi 32 Duniani ambazo zimethibitishwa na Shirika la Umoja wa Mataifa  kuweka jitihada kubwa za kupunguza kiwango cha maambukizi mapya ya UKIMWI kwa Asilimia 25. Mafanikio hayo yanatia moyo kwamba mkazo unaotiliwa na Serikali na Wadau wengine umeanza kuzaa Matunda. Hata hivyo, jitihada zaidi zitahitajika kutoka kila Sekta, Asasi Zisizo za Serikali, Wananchi na Watu Binafsi katika Mapambano Dhidi ya VVU na UKIMWI.

102.      Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/2012, Serikali imeweka jitihada kubwa za kuendelea kupunguza Maambukizi Mapya, Vifo vitokanavyo na UKIMWI na Unyanyapaa. Hadi Desemba 2011, jumla ya watu 1,125,211 wamepata huduma na Ushauri Nasaha na Upimaji  wa VVU kwa hiari. Aidha, Watu wanaoishi na VVU wapatao 412,108 wanapata Dawa za ARV’s chini ya Mpango wa Taifa wa Matunzo na Matibabu. Katika mwaka 2012/2013,  Serikali itaimarisha Uratibu wa shughuli za UKIMWI hasa katika Asasi za Kiraia na kuongeza juhudi za uraghibishaji na uhamasishaji kwa Umma. Serikali pia itaandaa Mkakati wa Tatu wa Kitaifa wa Mapambano dhidi ya UKIMWI na kufanya mapitio ya Mkakati wa Kinga Nchini.

Dawa za Kulevya


103.      Mheshimiwa Spika, Serikali imejizatiti kukabiliana na tatizo la usafirishaji na matumizi ya Dawa za Kulevya nchini. Katika kipindi cha Julai 2011 hadi Februari 2012, Kilo 349 za  Dawa za Kulevya za Viwandani,  Kilo 48,227 za  Bangi  na  Kilo  10,680  za  Mirungi  zilikamatwa. Hali hii si  nzuri  na  ni  dalili tosha kuwa nguvu zaidi zinahitajika ili kukabiliana na janga hili kubwa kwa Jamii yetu. Serikali itaendelea kutoa Elimu kwa Umma juu ya madhara ya Dawa za Kulevya, kufanya misako na operesheni katika maeneo mbalimbali na kuendelea kuteketeza mashamba ya bangi. Aidha, Serikali itaimarisha na kuboresha Huduma za Tiba na Utengemao kwa Waathirika wa Dawa za Kulevya. Napenda kuwatahadharisha wale wote wanaojihusisha na biashara hiyo haramu kwamba Tanzania siyo Kituo cha Kupitisha au sehemu ya kufanyia Biashara ya Dawa za Kulevya. Vyombo vya Usalama vimeimarishwa ili kudhibiti Biashara hiyo. Nachukua fursa hii kukishukuru na kukipongeza Kikosi Maalum cha Serikali cha Kupambana na Dawa za Kulevya ambacho kimefanya kazi kubwa  ya  kukamata dawa nyingi zilizoingizwa Nchini. Nawasihi waendelee kufanya kazi hiyo kwa moyo zaidi ili kuepusha Nchi yetu na athari kubwa zitokanazo na matumizi ya Dawa za Kulevya.

 

Ustawishaji wa Makao Makuu Dodoma


104.      Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/2012, Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Dodoma imefanya Mapitio ya Mpango Kabambe wa Kuendeleza Mji Mkuu Dodoma ili kuzingatia kasi ya ukuaji wa Mji huo. Aidha, mapitio ya Ikama  na  Muundo wa Utumishi umefanyika kwa lengo la  kuongeza ufanisi  wa kiutendaji wa Mamlaka. Kazi nyingine zilizofanyika ni ujenzi wa Barabara zenye urefu wa Kilomita 27 katika maeneo ya Ipagala, Area E, Chang’ombe Extension, Mwangaza, Chidachi na inaendelea na ujenzi wa Barabara zenye urefu wa Kilomita 15 kwa kiwango cha Lami katika maeneo ya Kisasa na Chang’ombe. Aidha, Mamlaka imepata Mkopo kutoka Benki ya CRDB wa jumla ya Shilingi Bilioni 16 kwa ajili ya uwekaji wa miundombinu ya maji, umeme na barabara zenye jumla ya urefu wa Kilomita 20.6 kwa kiwango cha Lami katika eneo la Uwekezaji la Njedengwa.

105.      Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2012/2013, Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu itafanya kazi ya kusanifu Mipango ya Makazi ya Uendelezaji wa Miji (Satellite Towns) katika maeneo ya Ihumwa na Hombolo. Mamlaka pia itaendelea kupima Viwanja 7,850 katika maeneo ya Iyumbu, Nzuguni na Miganga na kukamilisha upimaji wa viwanja vya zamani 1,938 katika maeneo ya Ipagala, Nkuhungu na Kisasa. Hali kadhalika, Mamlaka itajenga barabara zenye urefu wa Kilomita 11.3 kwa kiwango cha Lami katika maeneo ya Area ‘A’ na Kikuyu na kuendelea na ujenzi wa miundombinu ya maji, umeme na barabara kwa kiwango cha Lami katika eneo la Uwekezaji la Njedengwa. Serikali pia itafanyia kazi mapendekezo ya Mshauri Mwelekezi aliyefanya mapitio ya Muundo wa CDA hasa kutatua mwingiliano wa utendaji uliopo kati ya CDA na Manispaa ya Dodoma.

 

Mpango wa Uendeshaji wa Shughuli za Serikali kwa Uwazi


106.      Mheshimiwa Spika, mwezi Novemba 2011, nililiarifu Bunge lako Tukufu kwamba Tanzania imejiunga na Mpango wa Kimataifa wa Uendeshaji wa Shughuli za Serikali kwa Uwazi (Open Government Partnership – OGP). Mpango huo unahimiza uendeshaji wa shughuli za Serikali kwa Uwazi, Utawala Bora, Uadilifu, Mapambano Dhidi ya Rushwa na Ushirikishwaji mpana wa Wananchi katika Mipango ya maendeleo na usimamizi bora wa Rasilimali za Taifa. Chini ya makubaliano ya Mpango huo, kila Nchi inaandaa Mpango Kazi wa Utekelezaji ambao ni shirikishi na unaotekelezeka kulingana na mazingira yake. Napenda kuliarifu Bunge lako kuwa Serikali imeandaa Mpango Kazi wa utekelezaji ambapo Sekta za Afya, Elimu na Maji zimepewa kipaumbele. Mpango Kazi huo uliwasilishwa katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Viongozi wanaohusika na Mpango huo uliofanyika tarehe 17-18 Aprili 2012, Nchini Brazil. Utekelezaji wa Mpango huo utaanza katika mwaka 2012/2013.

UDHIBITI WA MATUMIZI YA SERIKALI


107.      Mheshimiwa Spika, katika Mkutano wa Saba wa Bunge mwezi Aprili 2012, niliahidi kuwa Serikali itayafanyia kazi maoni, ushauri na mapendekezo yaliyotolewa na Waheshimiwa Wabunge wakati wakijadili Taarifa mbalimbali  za  Kamati  za  Kudumu  za Bunge. Taarifa hizo ni  pamoja  na  zile  za  Kamati zinazoshughulikia Hesabu  za  Serikali  Kuu,  Mashirika ya Umma na Mamlaka za Serikali  za Mitaa  ambazo  ziliainisha  Hoja  mbalimbali  za Ukaguzi  uliofanywa na Mdhibiti na  Mkaguzi Mkuu  wa  Hesabu   za   Serikali  kwa   mwaka  2009/2010. Aidha, nilieleza kuwa Serikali itawawajibisha wote waliotajwa kuhusika na ubadhirifu wa Mali ya Umma ulioainishwa katika Taarifa hizo pale itakapothibitika kuwa Watumishi hao wametenda makosa.

108.       Mheshimiwa Spika, Serikali imeziagiza Mamlaka za Serikali za Mitaa kupitia Taarifa na Hoja zote za Ukaguzi za mwaka 2009/2010, zilizotolewa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na kuzitafutia majibu fasaha katika kipindi cha miezi mitatu kuanzia mwezi Aprili 2012. Baada ya zoezi hilo kukamilika, Taarifa hizo zitawasilishwa Ngazi ya Mkoa ambapo watapitia majibu ya Hoja hizo na kuziwasilisha katika Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC). Taarifa za Mikoa na Halmashauri zote zitawasilishwa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kabla ya mwezi Novemba 2012 ili hatimaye kuandaa majibu ya pamoja na kuyawasilisha Bungeni.

109.      Mheshimiwa Spika, vilevile, Wizara, Wakala, Mashirika ya Umma na Idara za Serikali Zinazojitegemea zimeagizwa  kupitia  Hoja  zote  zilizotolewa  na  Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na kuzifanyia kazi. Wakala wa Serikali na Mashirika ya Umma yametakiwa kupitisha majibu ya Hoja kwenye Bodi za Wakurugenzi kabla ya kuwasilishwa Wizarani. Utaratibu huo  utakuwa  endelevu  na  utafanyika  kila  mwaka. Lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa Usimamizi wa Fedha za Umma unaimarishwa katika Ngazi zote. Majibu ya Hoja zote yatawasilishwa Bungeni ili kuongeza Uwazi na Uwajibikaji wa Fedha za Umma.

110.      Mheshimiwa Spika, sambamba na hatua hiyo, Watumishi  wa Umma watakaotuhumiwa kufanya ubadhirifu  wa  fedha  za Umma watachunguzwa na tuhuma  zikibainika  ni za kweli watavuliwa madaraka waliyo nayo na kufikishwa katika Vyombo vya Sheria. Napenda kusisitiza kwamba, Serikali haitawahamisha Watumishi wa aina hiyo, bali hatua za kinidhamu na kisheria zitachukuliwa wakiwa kwenye vituo vyao vya kazi. Natoa wito kwa Watendaji Wakuu wa Serikali, Bodi za Wakurugenzi wa Mashirika ya Umma na Madiwani kuhakikisha wanashiriki ipasavyo katika kusimamia fedha za Umma kwa mujibu wa Sheria, Taratibu, Miongozo na Kanuni zilizopo. Nawaagiza Wakurugenzi Watendaji wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kubandika kwenye mbao za matangazo za Makao Makuu ya Halmashauri na katika vituo vyote vya utoaji huduma kiasi cha fedha kinachopokelewa kila mwezi na matumizi yake. Hii itawezesha Wananchi kufuatilia matumizi ya fedha zilizopelekwa kwa ajili ya utoaji huduma kwenye maeneo yao.

111.      Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuchukua hatua madhubuti za kupunguza matumizi yasiyo na tija, hususan ununuzi wa magari makubwa na ya kifahari ambayo  gharama za ununuzi na uendeshaji ni kubwa sana. Kuanzia mwaka 2012/2013, hatua zaidi zitachukuliwa kwa kuweka ukomo wa ukubwa wa injini wa magari ambayo yanaweza kununuliwa na Serikali Kuu na Taasisi zake pamoja na Mamlaka za Serikali za Mitaa. Chini ya utaratibu huo, magari yatakayonunuliwa yatakuwa ni yale yasiyozidi ukubwa wa injini wa CC 3,000 kwa Viongozi na  Watendaji  Wakuu na yasiyozidi CC 2,000 kwa Watumishi wengine ambao wana stahili ya kutumia magari ya Serikali. Vilevile, ili kupunguza matumizi ya magari kwa Viongozi na Watendaji Wakuu kwa safari za Mikoani, Serikali itaanzisha vituo vya Kanda vya magari ya Serikali au kila Ofisi itatenga magari machache yatakayotumika Mikoani kwa shughuli za kikazi. Mwongozo wa utekelezaji utatolewa. Inategemewa kuwa utaratibu huu utapunguza matumizi ya fedha za Serikali kwa kiwango kikubwa.

HITIMISHO


112.      Mheshimiwa Spika, nimeelezea kwa muhtasari baadhi ya shughuli ambazo Serikali imetekeleza kwa kipindi kilichopita. Aidha, nimetoa Mwelekeo wa Kazi zitakazofanyika mwaka 2012/2013. Kwa kuhitimisha, napenda kusisitiza mambo muhimu yafuatayo:

a)        Wote tunatambua kuwa tumeanza kutekeleza Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kwa Tume ya Kuratibu maoni kuanza kazi. Tuendelee kuwaelimisha Wananchi kuhusu Mambo ya Msingi wakati wa kuchangia Maoni, na kwamba kila mmoja anao wajibu na Uhuru wa kutoa Maoni yake kwenye Tume bila shinikizo lolote.        

b)       Tumepitisha Bajeti ya Serikali ambayo changamoto yake kubwa ni Rasilimali Fedha kidogo tuliyonayo kukidhi mahitaji makubwa ya kutoa huduma bora kwa Wananchi tunaowaongoza. Kutokana na hali hiyo, ni muhimu kujipanga vizuri kudhibiti na kusimamia matumizi ya  fedha  za  Umma  kwa  ufanisi   na   tija   zaidi. Serikali itaimarisha Mifumo yake ya usimamizi na ufuatiliaji na kuhakikisha kwamba fedha za umma zinatumika kulingana na Sheria na Kanuni za Matumizi ya Fedha za Serikali.
     
c)        Katika muda usiozidi miezi miwili ijayo, tarehe 26 Agosti 2012 itakuwa ni Siku ya Sensa ya Watu na Makazi Nchini. Napenda kusisitiza kwamba uandikishaji hautakuwa wa siku moja tu, bali siku hiyo ndiyo itakayokuwa msingi wa kuhesabu watu waliolala katika Kaya husika. Kazi hiyo itaendelea kwa  siku saba hadi tarehe 2 Septemba 2012. Natoa wito kwa Wananchi kutoa ushirikiano kwa Makarani wa Sensa na kujitokeza kuhesabiwa na kuhakikisha kwamba kila mtu anahesabiwa mara moja tu. Aidha, Viongozi katika Ngazi zote wana wajibu mkubwa wa kuwahamasisha Wananchi kuhusu umuhimu wa kushiriki kwenye Sensa.

113.      Mheshimiwa Spika, kabla  ya kumaliza Hotuba yangu, nimwombe Mheshimiwa Hawa Abdulrahman Ghasia (Mb.), Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa atoe maelezo ya Mapitio ya Kazi  zilizofanyika  katika  mwaka  2011/2012  na Mwelekeo  wa Kazi za Tawala  za  Mikoa  na  Serikali za Mitaa kwa mwaka 2012/2013. Ni matumaini yangu kwamba maelezo hayo yatawezesha Waheshimiwa Wabunge na Wananchi kufahamu kwa upana shughuli zinazotekelezwa na Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa.

 

SHUKRANI


114.      Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii sasa kuwashukuru Mawaziri na Naibu Mawaziri kwa ushirikiano walionipa katika kipindi hiki. Aidha, nawashukuru Watumishi wote wa Serikali na Taasisi zake chini ya Uongozi wa Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi  Ombeni Yohana Sefue kwa kukamilisha Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2012/2013. Nawashukuru Watanzania wote na Washirika wetu wa Maendeleo kwa Michango yao ambayo imewezesha Serikali kutoa huduma mbalimbali kwa Wananchi.

115.       Mheshimiwa Spika, vilevile, napenda kuwashukuru Mheshimiwa William Vangimembe Lukuvi, Mbunge wa Ismani, Waziri wa Nchi (Sera, Uratibu na Bunge); Mheshimiwa  Dkt. Mary Michael Nagu, Mbunge wa Hanang, Waziri wa Nchi (Uwekezaji na Uwezeshaji); Mheshimiwa Hawa Abdulrahman Ghasia, Mbunge wa Mtwara Vijijini, Waziri wa Nchi, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa; Mheshimiwa  Aggrey Joshua Mwanry, Mbunge wa Siha, Naibu Waziri, Ofisi  ya  Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa; na Mheshimiwa Majaliwa Kassim  Majaliwa,   Mbunge  wa  Ruangwa,  Naibu  Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Elimu) kwa ushirikiano walionipa katika utekelezaji wa majukumu ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Shukrani za pekee kwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya kwa jitihada walizoonesha katika kipindi hiki. Nawashukuru vilevile Wafanyakazi wote wa Ofisi ya Waziri Mkuu, chini ya Uongozi wa Makatibu Wakuu, Bwana Peniel Moses Lyimo na Bwana Hussein Athuman Kattanga na Naibu Makatibu Wakuu, Bwana Charles Amos Pallangyo, Jumanne Abdallah Sagini na Alphayo Japan Kidata kwa ushauri wao wa Kitaalam ambao wamenipa mimi na Waheshimiwa Mawaziri wa Nchi katika kipindi hiki. Nawashukuru kwa kukamilisha maandalizi yote ya Makadirio ya Matumizi ya Fedha ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka 2012/2013.

116.        Mheshimiwa Spika, kipekee napenda nimshukuru Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa imani yake kwangu na kuendelea kuniwezesha kutekeleza majukumu yangu ipasavyo. Pia, ninamshukuru Mheshimiwa Dkt. Mohamed Gharib Bilal, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa  Tanzania  na  Mheshimiwa  Dkt.  Ali  Mohamed  Shein, Rais  wa  Zanzibar  na  Mwenyekiti  wa Baraza la Mapinduzi kwa ushirikiano mkubwa wanaonipa katika kuwatumikia Watanzania. Vilevile, ninawashukuru Waheshimiwa Wabunge, Viongozi wote wa Kitaifa na wa ngazi nyingine zote kwa ushirikiano wanaonipa katika kutekeleza majukumu yangu. Kwa umuhimu wa kipekee, napenda kuwashukuru Wapiga Kura wangu kwa imani na ushirikiano wanaoendelea kunipa katika kuleta maendeleo ya Jimbo la Katavi. Naomba pia nitumie fursa hii kumshukuru sana sana Mama Tunu Pinda kwa uvumilivu wake na msaada mkubwa anaonipa katika kutekeleza majukumu yangu mazito. Vilevile, nawashukuru sana Watoto wangu ambao mara nyingi wamekuwa wakinitia moyo na wamekuwa na uvumilivu mkubwa wanaponikosa kwa sababu ya kazi. Wote nasema, Asanteni sana kwa kunipa nguvu ya kutekeleza majukumu yangu. Nyote nawashukuru sana!

MAKADIRIO YA  MATUMIZI  YA  FEDHA  YA OFISI  YA  WAZIRI MKUU, OFISI YA  WAZIRI MKUU - TAWALA  ZA  MIKOA  NA  SERIKALI  ZA MITAA NA OFISI YA BUNGE  YA MWAKA 2012/2013


117.        Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2012/2013, Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi zake inaliomba Bunge lako Tukufu liidhinishe jumla ya Shilingi Bilioni Mia Moja Sabini na Sita, Milioni Mia Saba Tisini na Nne, Laki Nane Thelathini na Nane Elfu (176,794,838,000). Kati ya fedha hizo, Shilingi Bilioni Sitini na Nane, Milioni Mia Tano Ishirini na Mbili, Laki Nane Sitini na Sita Elfu (68,522,866,000) ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na Shilingi Bilioni Mia Moja na Nane, Milioni Mia Mbili Sabini na Moja, Laki Tisa Sabini na Mbili Elfu (108,271,972,000)  ni kwa ajili ya Mpango wa Maendeleo.

118.         Mheshimiwa Spika, vilevile, kwa mwaka 2012/2013, Ofisi ya Waziri Mkuu - Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Asasi zake inaombewa jumla ya Shilingi Bilioni Mia Moja Themanini na Sita, Milioni Mia Nane Tisini na Moja, Laki Tano Tisini na Nane Elfu (186,891,598,000). Kati ya fedha hizo, Shilingi Bilioni Mia Moja Sitini na Nne, Milioni Mia Sita Kumi na Nne, Laki Saba Ishirini na Sita  Elfu  (164,614,726,000)  ni  kwa  ajili  ya  Matumizi ya Kawaida na Shilingi Bilioni Ishirini na Mbili, Milioni Mia Mbili Sabini na Sita, Laki Nane Sabini na Mbili Elfu (22,276,872,000) ni kwa ajili ya Matumizi ya Maendeleo.

119.        Mheshimiwa Spika, Ofisi za Wakuu wa Mikoa zinaombewa jumla ya Shilingi Bilioni Mia Moja Sabini na Tatu, Milioni Mia Mbili Sabini na Sita, Laki Saba Sitini na Moja Elfu (173,276,761,000). Kati ya fedha hizo, Shilingi Bilioni Mia Moja Arobaini na Sita, Milioni Mia Tano Hamsini na Mbili, Laki Mbili Sitini na Mbili Elfu (146,552,262,000) ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na Shilingi Bilioni Ishirini na Sita, Milioni Mia Saba Ishirini na Nne, Laki Nne Tisini na Tisa Elfu (26,724,499,000) ni kwa ajili ya Matumizi ya Maendeleo. Aidha, Halmashauri zote zinaombewa jumla ya Shilingi Trilioni Tatu, Bilioni Mia Mbili Sabini na Tisa, Milioni Mia Nane; na Sabini na Tano Elfu (3,279,800,075,000). Kati ya fedha hizo, Shilingi Trilioni Mbili, Bilioni Mia Saba Thelathini na Tano, Milioni Mia Sita Arobaini na Sita, Laki Moja Kumi na Saba Elfu (2,735,646,117,000) ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na Shilingi Bilioni Mia Tano Arobaini na Nne, Milioni Mia Moja Hamsini na Tatu, Laki Tisa Hamsini na Nane Elfu (544,153,958,000) ni kwa ajili ya Matumizi ya Maendeleo.

120.         Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Bunge la Jamhuri ya Muungano inaombewa jumla ya Shilingi Bilioni Mia Moja Kumi na Tatu, Milioni Mia Mbili Ishirini, Laki Sita Hamsini na Tatu Elfu (113,220,653,000) kwa ajili ya Mfuko  wa  Bunge  ambapo  Shilingi Bilioni Mia Moja Kumi na Moja, Milioni Mia Tano Themanini na Tano, Laki Sita Hamsini na Tatu Elfu (111,585,653,000) ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na Shilingi Bilioni Moja na Milioni Mia Sita Thelathini na Tano (1,635,000,000) ni kwa ajili ya Matumizi ya Maendeleo.

 

MUHTASARI


121.         Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo haya kwa muhtasari, naomba sasa Bunge lako Tukufu likubali kuidhinisha Makadirio ya Matumizi ya Fedha kwa mwaka 2012/2013 ya jumla ya Shilingi Bilioni Mia Moja Kumi na Tatu, Milioni Mia Mbili Ishirini, Laki Sita Hamsini na Tatu Elfu (113,220,653,000) kwa ajili ya Mfuko wa Bunge, na jumla ya Shilingi Trilioni Tatu, Bilioni Mia Nane Kumi na Sita, Milioni Mia Saba Sitini na Tatu, Laki Mbili Sabini na Mbili Elfu (3,816,763,272,000) kwa ajili ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Waziri Mkuu - Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ikiwa ni Matumizi ya Kawaida na Fedha za Maendeleo za Ndani na Nje kwa ujumla wake.

122.        Mheshimiwa Spika, pamoja na Hotuba hii, yapo Majedwali ambayo yanafafanua kwa kina Makadirio ya Matumizi ya Fedha ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi zake, Ofisi ya Waziri Mkuu - Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Bunge.

123.        Mheshimiwa Spika, naomba kutoa Hoja.

2 Comments:

Unknown said...

Je, wewe katika haja ya mkopo? Je, unataka kuwa na utulivu wa kifedha? Au unataka kupanua biashara yako? Tunatoa kampuni mkopo, mkopo auto, mikopo ya biashara, na mkopo binafsi, christmass mkopo kupunguzwa sana kiwango cha riba ya 2% kwa muda vizuri ambayo ni negotiable. Kutoa hii ni wazi kwa wote ambayo itakuwa na uwezo wa kulipa nyuma katika wakati. Kindly kupata nyuma na sisi kama nia na email hii: mauricefinance@hotmail.com
Barua pepe: mauricefinance@hotmail.com

Unknown said...

Salamu Kila moja.

i am Mr Paul Williams binafsi mkopo Taasisi, sisi ni vyombo vya kibinafsi kutoa kila aina ya mikopo kwa watu ambao ni kifedha chini na katika mahitaji ya msaada wa kifedha, sisi kutoa mikopo kwa kiwango nafuu sana bila matatizo yoyote. kampuni yetu ni vizuri kusajiliwa na uwezo wa kutoa mikopo kwa watu binafsi na kushirikiana miili katika mazingira mazuri. huduma zetu ni haraka na rahisi. kama wewe ni nia ya kupata mkopo kutoka kwetu kindly wasiliana nasi juu ya kampuni yetu email: paulwilliamsfinance@gmail.com

kutembelea sisi leo kwa ajili ya huduma zetu za kuaminika
Regards
Mr Paul Williams.
Kampuni pepe: paulwilliamsfinance@gmail.com
Wasiliana nasi sasa.

Post a Comment