HABARI

 

Friday, June 29, 2012

BAN KI MOON AMUAGA RASMI DK. ASHA-ROSE MIGIRO

0 Comments
Na Mwandishi Maalum, NEW YORK

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, amemteua  Naibu Katibu Mkuu anayemaliza muda wake, Dkt, Asha-Rose Migiro kuwa  mjumbe wake maalum katika masuala ya ukimwi na ugonjwa wa ukimwi Barani Afrika.
Ban Ki Moon ametangaza uteuzi huo wakati wa hafla maalum aliyoiandaa mahsusi kwaajili ya kumuaga  Naibu Katibu Mkuu wake,ambaye anahitimisha  utumishi wake wa  miaka mitano na nusu   katika nafasi ya Unaibu katibu Mkuu.
Hafla hiyo imefanyika   siku ya alhamisi katika viunga vya Umoja wa Mataifa, na kuhudhuriwa na wageni waalikwa  mbalimbali wakiwamo mabalozi na wakuu wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa.
“Ninatangaza rasmi kwamba ninamteua dkt.  Asha- Rose Migiro kuwa  mjumbe wangu maalum katika masuala ya ukimwi na ugonjwa wa Ukimwi Barani  Afrika. Akasema  Ban Ki Moon tangazo lililoshangiliwa kwa nguvu na wageni waalikwa.
Akiongea kwa hisia, Ban Ki Moon, ameeleza kwamba ingawa Migiro alikuwa naibu katibu mkuu wake, lakini amekuwa mwalimu wake, amejifunza mengi toka kwake na daima ataendelea kuenzi mchango wake mkubwa.
“ Kama ni kuvaa viatu vyake, naweza kusema ningechekesha sana,  kwa ufupi siwezi kuvaa viatu vya Migiro, amekuwa msaada mkubwa sana kwangu, ameniwakilisha vema kila mahali nilipomtuma  hata katika mazingira magumu na ya hatari,  kote ameniwakilisha vema sana, kama  mwalimu wangu, na kama profesa wangu anastahili alama ya juu sana” akasema  Ban Ki Moon na kushangiliwa.

Akamuelezea  Migiro kama kiongozi si tu mwadilifu, lakini mwanadiplomasia  aliyebobea, aliyefanya kazi kubwa,ngumu na nzito kwa moyo mkunjufu, uhodari , umakini, na uadilifu wa hali ya juu sana.
“  Siyo rahisi kuelezea yale aliyoyafanya nyuma ya pazia, namna gani alivyochapa kazi kwa nguvu,  yapo mengi makubwa ambayo Migiro ameyafanya na  kuyakamilisha kwa uadilifu wa hali ya juu. Migiro ni mwanadiplomasia aliyebobea lakini ni mtu wa vitendo, vitendo ambavyo lazima utaona matunda yake” akabainisha Ban Ki Moon
Na kuongeza “  Migiro  amefanya kazi na viongozi wagumu,  kiwamo aliyekuwa  Rais wa Libya Muammar  Quadaff aliyethubutu hata kumrushia katiba ya Umoja wa Mataifa, amezikuna nyonyo za watu wengi wakiwamo watu wanyonge na wenye matatizo mbalimbali. Migoro  unaondoka, lakini Umoja wa  Mataifa  hauta sahau mchango wako. Hapa ni nyumbani kwako, na nitaendelea kuomba msaada wako na ushirikiano wako, bado nitaendelea kukuhitaji” akasisitiza Ban Ki Moon
 Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa,  akatumia fursa hiyo kuishukuru serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  kwa kumruhusu Migiro kwenda kuitumikia jumuia ya kimataifa.
“ Ninapenda  kutoa shukrani zangu za pekee kwa  jamhuri ya muungano wa Tanzania, kwa kumtoa Migiro katika utumishi wake wa Umma kuja kunisaidia , kwa serikali ya Tanzania na  watanzania nasema asanteni sana” akasema Ban Ki Moon..
Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu dkt. Asha-Rose Migiro amesema anaupokea kwa mikono miwili uteuzi wa kuwa mjumbe maalum wa Katibu Mkuu katika masuala ya Ukimwi.
Akasema   masuala ya  ukimwi na ugonjwa wa ukimwi, ni eneo ambalo limo ndani ya moyo wake  na kwamba anashukuru kuona kwamba Katibu Mkuu anamuamini kwamba anaweza kumsaidia. Akaahidi kwam atalitekeleza  jukumu  hilo kwa  heshima  kubwa.
Akamshukuru Ban Ki Moon, kwa kumuamini kwamba anaweza kumsaidia kama naibu Katibu Mkuu, na akamshukuru pia kwa ushirikiano mkubwa na uhusiano mkubwa uliojengeka kati yake na Ban Ki Moon lakini pia kati yake na wasaidizi wake.  Ushirikiano ambao anasema ulichagiza utendaji kazi  kufanikisha dira na matarajio ya  Katibu Mkuu.
“Katibu Mkuu amenipa heshima ya kihistoria, heshima ya kuwa msadizi wake,  ni heshima kubwa kwangu na kwa yeyote atakayekuja kuandika historia yangu, kwa namna yoyote ile hawezi kukwepa  kumtaja  Ban Ki Moon, naomba nikushukuru sana kwa heshima hii kubwa uliyonipa” akasema Migiro.
Hafla hiyo pia imehudhuriwa  na familia ya Naibu Katibu Mkuu ikijumuisha  mume wake, Profesa  Cleophas Migiro,  mdogo wa  Naibu Katibu Mkuu, Bi. Amina  Mtengeti na mtoto wa  mwisho wa Migiro Chansa Jasmin.
Naibu Katibu Migiro anakuwa mwanamke wa pili kushika wadhifa huo na mwanamke mwafrika wa kwanza. Lakini pia ni naibu katibu mkuu ambaye amehudumu katika wadhifa huo kwa miaka mitano na nusu.

0 Comments:

Post a Comment